Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) imefanya mabadiliko madogo ya Sekreterieti ya Halmashauri hiyo Taifa kwa kuwachagua wajumbe akiwemo Amos Gabriel Makalla kuwa Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Itikadi, Uenezi na Mafunzo. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Makala amechukua nafasi ya Paul Makonda ambaye ameteuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha ambaye amehudumu katika nafasi hiyo kwa miezi mitano.
Pia katika kikao maalum cha Halmashauri hiyo kilichoongozwa na Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, pamoja na masuala mengine, imemchagua John Mongella kuwa Naibu Katibu Mkuu wa CCM Bara.
Mongela amechukua nafasi ya Anamringi Macha ambaye aliteuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga.
Halmashauri hiyo iliyoketi leo Jumatano jijini Dar es Salaam pia imemchagua Ally Salum Hapi kuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Wazazi Tanzania.
Hapi amechukua nafasl ya Gilbert Kalima ambaye ameteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Mkinga.
“Jokate Urban Mwegelo kuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa CCM, akichukua nafasi ya Ndugu Fakii Raphael Lulandala ambaye ameteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro,” imesema taarifa ya Halmashauri hiyo.
Aidha, katika kikao hicho, Halmashauri Kuu ya CCM Taifa imezipongeza Serikali zake zote mbili, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, chini ya Rais Samia na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, chini ya Rais Dk. Hussen Ali Mwinyi, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, kwa kazi kubwa na nzuri ya kuendelea kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2020- 2025.
Leave a comment