Viongozi sita wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wamefariki dunia na wengine 11 kujeruhiwa katika ajali ya gari ya abiria Toyota Haisi lenye namba za usajili T 733 BBP baada ya kupinduka katika kijiji cha Ndulamo wilaya ya Makete mkoani Njombe. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Ajali hiyo imetokea usiku wa kuamkia leo Jumamosi baada ya dereva wa gari hilo kushindwa kukata kona.
Aidha, pia imeelezwa kuwa makada hao walikuwa wakitoka kwenye mkutano wa mlezi wa chama hicho mkoa wa Njombe, Halima Mohamed Mamuya uliyokuwa ukifanyika wilayani humo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Njombe John Makuri Imori amethibitisha kutokea kwa vifo hivyo katika ajali ya gari hiyo iliyokuwa ikitokea Makete kuelekea Tandala.
Amesema katika gari hilo lililokuwa na abiria 18, kati ya sita waliofariki, watatu ni wanaume na watatu ni wanawake).
Ameongeza kuwa chanzo cha ajali ni mwendokasi uliomfaya dereva kushindwa kulimudu gari hilo lililokuwa katika mteremko mkali.
Aidha, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Juma Mfanga amesema majeruhi wengi wamevunjika viungo na wanaendelea na matibabu katika Hospitali ya Ikonda.
Amesema wengine wanaendelea na matibabu katika Hospitali ya Wilaya ya Makete ambapo pia tayari madaktari wengine kutoka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe wamefika katika Hospitali hizo kuongeza nguvu.
Leave a comment