RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, ameshiriki misa ya kumuombea Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, aliyefariki dunia tarehe 14 Oktoba 1999. Anaripoti Mwandishi Wetu, Manyara…(endelea).
Misa hiyo imefanyika leo tarehe 14 Oktoba 2023, katika Kanisa Katoliki Parokia ya Roho Mtakatifu Babati mkoani Manyara na kuongozwa na Mhashamu Baba Askofu wa Jimbo Katoliki la Mbulu, Antony Gasper Lwagen.
Mbali na Rais Samia, viongozi wengine walioshiriki misa hiyo ambayo inaenda sambamba na kumbukizi ya miaka 24 ya kifo cha Mwalimu Nyerere, ni Makamu wa Rais, Dk. Phillip Mpango. Naibu Waziri Mkuu, Dotto Biteko. Jaji Mkuu wa Tanzania, Prof. Ibrahim Juma na Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson.
Wengine ni Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana.
Akizungumza wakati anaongoza misa hiyo, Askofu Lwagen aliwataka watanzania kumuombea Mwalimu Nyerere ili Mungu ampe pumziko la milele.
“Adhimisho hili ni la muhimu sana la kitaifa linalohusu kumbukizi ya siku ya kifo cha Mwalimu Nyerere, kwa namna ya kipekee naomba tumuombee na tutoe shukrani kwa Mungu kwa zawadi ya maisha yake ambayo imetufadhili kwa mengi,” amesema Askofu Lwagen na kuongeza:.
“Tunatumia nafasi hii kuiombea nchi yetu na raia wote tubaki kuwa na umoja, amani na mshikamano siku zote. Tunawaombea viongozi wetu wote wa dini na serikali kwa namna ya kipekee rais wetu Mungu aendelee kumpa afya na nguvu amjalie busara anayohitaji.”
Akizungumza kwa niaba ya Rais Samia, Dk. Mpango amesema watanzania wanamshukuru Mungu kwa zawadi wa Mwalimu Nyerere ambaye ni mwasisi wa uhuru, amani na mshikamano wa taifa.
“Tukumbuke wajibu wetu kwa taiofa letu, ndiyo namna bora ya kumuenzi na kubwa zaidi kulinda uhuru wa taifa lakini kukataa aina yoyote ya unyonyaji na ukandamizaji,” amesema Dk. Mpango.
Leave a comment