WAZIRI wa Maliasili na Utalii nchini Tanzania, Balozi Pindi Chana amewaomba Watanzania kujitokeza katika maadhimisho ya kusherehekea miaka 100 ya Urithi wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Maadhimisho hayo yatafanyika tarehe 13 Aprili 2022, Butiama mkoani Mara na mgeni rasmi atakuwa Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa.
Akizungumza jana Jumapili, tarehe 10 Aprili 2022, jijini Dodoma, Balozi Chana alisema lengo la maadhimisho hayo yanafanywa na wizara kwa kushirikiana na wadau mbalimbali na mkoa wa Mara ni kuenzi na kusherekea mchango maridhawa alioutoa Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere katika nyanja mbalimbali kitaifa na Kimataifa
Balozi Chana alisema maadhimisho hayo ni moja ya sehemu ya kutekeleza mpango wa miaka 10 wa kuenzi Urithi wa maisha ya Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere.
Lengo ni kuwashirikisha wadau ili kujenga uelewa wa pamoja kuhusu mchango wake na umuhimu wa kumuenzi, kukusanya, kuendeleza, kuhifadhi na kutangaza rasilimali za urithi wa Mwalimu Nyerere kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho ili kukuza na kuedeleza utalii.
“Tarehe 13 Aprili, 1922 ndiyo siku aliyozaliwa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na kama angekuwa hai tarehe 13 Aprili, 2022 angetimiza miaka 100, hivyo tunasherehekea kuenzi urithi wa maisha ya Hayati Baba wa Taifa,” alisema Balozi Chana
Aliwaalika wananchi na wadau mbalimbali wakiwemo waandishi wa habari kushiriki kikamilifu katika maadhimisho hayo ya kumuenzi Baba wa Taifa, Mwalimu Julius kambarage Nyerere ambapo maandalizi ya maadhimisho hayo yanafanywa na Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kushirikiana na uongozi wa mkoa wa Mara.
“Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kushirikiana na Mkoa wa Mara tunawaalika wananchi na wadau wote kushiriki kwenye kilele cha maadhimisho haya vilevile kuendelea kuenzi kwa vitendo Urithi wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere Baba wa Taifa letu,” alisema.
Aidha, alisema kuelekea kilele cha maadhimisho hayo matukio mbalimbali yanaendelea kufanyika ikiwa ni pamoja na mikutano ya wadau mbalimbali, mashindano ya baiskeli, matembezi ya hiari na midahalo inayoendeshwa na taasisi mbalimbali.
Pia, alisema wakati wa kilele cha maadhimisho hayo kutakuwa na burudani mbalimbali,programu za wanafunzi za kielimu, uzinduzi wa Mpango wa kuenzi Urithi wa Mwalimu Nyerere, nembo maalum ya Mwalimu@100 pamoja na onesho maalum la Mwalimu Nyerere.
Leave a comment