WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa, ametoa wito kwa taasisi za elimu nchini, kufanya utafiti juu ya mabadiliko ya teknolojia, ili kubaini fursa zake katika ukuzaji uchumi. Anaripoti Nasra Bakari, DMC … (endelea).
Waziri Majaliwa ametoa wito huo leo Jumatatu tarehe 24 Mei 2021, akifungua maadhimisho ya sita ya wiki ya utafiti na ubunifu, yakiyofanyika katika viwanja vya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Jijini Dodoma.
“Mabadiliko haya ya teknolojia yanatokea kwa kasi kubwa ulimwenguni, yanachochewa na mwenendo wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Hivyo basi, nasi hatunabudi kujipanga vyema kufanya tafiti, ili kuendana na kasi hiyo,” amesema Majaliwa.
Waziri Majaliwa amesema baada ya tafiti hizo kufanyika, waweke wazi matokeo yake ili umma wa Tanzania uweze kufaidika na matokeo hayo, kwa kupata suluhisho za changamoto mbalimbali.
“Wakati tukifanya hayo yote, ni muhimu pia kujitayarisha kutumia kikamilifu matokeo ya tafiti zetu, kama fursa au bidhaa adimu ya biashara,” amesema Majaliwa.
Aidha, Waziri Majaliwa amevitaka vyuo vikuu vyote nchini, kuweka utaratibu wa kufanya tafiti kisha kuonesha matokeo ya ke, ili kusaidia kuimarisha uhusiano wa karibu baina ya vyuo na soko la ajira.
Pia, Waziri Majaliwa ametoa wito kwa wamiliki wa viwanda kufadhili tafiti na bunifu mbalimbali, zinazohusiana na bidhaa zinazozalishwa na viwanda vyao.
“Tumieni vizuri wataalamu wa vyuo vyetu, kwani wanaweza kuleta majibu ya changamoto mbalimbali katika uzalishaji bidhaa, masoko ya bidhaa, mahitaji ya wateja na mambo mengine mengi,” amesema Waziri Majaliwa.
Kwa upande wake, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako, amesema wizara yake itaendelea kuimarisha tafiti, ili Taifa liweze kunufaika na teknolojia ya kisasa pamoja na kutoa huduma kwa jamii.
Leave a comment