WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa ameiagiza Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara kuunda jopo la wataalamu ili kufuatilia upandaji wa bei za bidhaa usioendana na uhalisia wa soko. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Amesema, wale wote watakaobainika kupandisha bidhaa hizo za ujenzi, vyakula, nishati na pembejeo za kilimo kinyume na bei halisi hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.
Majaliwa ametoa maagizo hayo leo Jumatano, tarehe 6 Aprili 2022, bungeni jijini Dodoma wakati akiwasilisha Bajeti ya Ofisi yake na Fungu la Bunge kwa mwaka wa fedha 2022/23.
Amesema, wizara hiyo ya uwekezaji inayoongozwa na Waziri Dk. Ashatu Kijaji ishirikiane na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) na Tume ya Ushindani (FCC) ifanye ufuatiliaji na tathmini ya mwenendo wa bei za bidhaa muhimu zinazozalishwa nchini na zile zinazotumia malighafi kutoka nje ya nchi.
Majaliwa amesema Serikali imechukua hatua mbalimbali ili kukabiliana na upandaji huo wa bidhaa muhimu. Hatua hizo ni pamoja na usimamiaji wa Sheria ya Ushindani Na. 8 ya Mwaka 2003 ambayo inazuia kupanga bei.
Amesema, hatua nyingine ni Serikali kutafuta vyanzo mbadala vya upatikanaji wa bidhaa na kuweka mifumo ya kusimamia masoko ya awali na minada.
“Serikali inawaelekeza wazalishaji na wasambazaji wa bidhaa muhimu kushusha mara moja bei za bidhaa walizopandisha pasipo kuendana na uhalisia wa soko ikiwa ni pamoja na kutotumia kipindi hiki cha mfungo wa Ramadhani na Kwaresma kupandisha bei,” amesema Majaliwa na kuongeza:
“Nawasihi wazalishaji na wafanyabiashara wa bidhaa muhimu kuuza bidhaa husika kwa kuzingatia gharama halisi za uingizaji, uzalishaji na usambazaji. Wale watakaobainika kupandisha bei bidhaa muhimu bila utaratibu hatua kali zitachukuliwa dhidi yao.”
Leave a comment