WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amesema serikali itaendelea kutoa fedha ili kukamilisha ujenzi wa Hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Songwe ili kuimarisha huduma za afya zikiwemo za kibingwa.
Amesema hospitali hiyo itakapokamilika itachochea utalii wa tiba kwa wagonjwa kutoka mataifa jirani ya Zambia na Malawi. Anaripoti Ibrahim Yassin, Songwe…(endelea).
Amebainisha hayo leo Alhamis baada ya kukagua na kuridhika na huduma zinazotolewa, ikiwemo maendeleo ya ujenzi wa baadhi ya majengo yanayoendelea kujengwa katika Hospitali hiyo ya Rufaa ya Mkoa wa Songwe.
Majaliwa alitembelea Hospitali hiyo iliyopo eneo la Hasamba, wilayani Mbozi na kuweka jiwe la msingi ikiwa ni siku ya kwanza ya ziara yake ya siku tatu mkoani hapa.
Amesema kuimarishwa kwa huduma za matibabu katika hospitali hiyo ambayo tayari imeanza kutoa huduma za kibingwa katika maeneo manne kutavutia wagonjwa kutoka mataifa hayo jirani ya Malawi na Zambia kuja kupata huduma katika Hospitali hiyo ya rufaa ya Mkoa wa Songwe.
“Hospitali hii inajengwa hapa Songwe ni ya kimkakati kwani mkoa huu umepakana na nchi jirani za Zambia na Malawi ambao wanakuja kutibiwa hapa, kwa vifaa vilivyopo hapa wagonjwa hawataenda kutibiwa hospitali ya kanda Mbeya na tutaiboresha zaidi”.
“Ndugu zetu hawa wa Malawi na Zambia kwa karibuni hawana huduma kubwa za kimatibabu kama zitakazotolewa hapa, maana yake ni nini wao watakuja hapa Mbozi kutibiwa kwa hiyo hapa tuna utalii wa matibabu” amesisitiza Waziri Mkuu.
Awali akitoa taarifa kwa Waziri Mkuu, Mkurugenzi mtendaji wa hospitali ya Rufaa Songwe (MOI), Dk. Juma Ramadhan Juma amesema hadi kufikia sasa ujenzi wa hospitali hiyo umetumia zaidi ya Sh. 16 bilioni ambapo kiasi cha Sh. 13 bilioni zimetumika kwa ajili ya ujenzi, hulu Sh. 3.289 bilioni zimetumika katika unuuzi wa vifaa tiba.
Dk. Juma aliongeza kuwa hospitali hiyo imeanza kutoa huduma za kibingwa katika maeneo makuu manne, ambayo ni huduma za kibingwa za macho, magonjwa ya wanawake na afya ya uzazi, huduma bingwa za magonjwa ya watoto pamoja na huduma ya dharura na ajali.
Aidha, Dk. Juma amesema kuwa katika kipindi cha Julai 2022 hadi Juni 2023 hospitali hiyo imehudumia wagonjwa 19,265 kati ya hao wagonjwa wa nje (OPD)17,929 na waliolazwa (IPD) ni 1336 kati ya hao kuna akina mama 695 waliojifungua salama hivyo kupunguza vifo vya akina mama vitokanavyo na uzazi na kufikia vitano.
Wakati huo huo, Naibu Waziri wa Afya Dk. Godwin Mollel amemueleza Waziri Mkuu kuwa ndani ya siku 21 wizara ya afya itakuwa imefunga mashine ya CT scan na mashine ya kisasa ya mionzi (digital x-ray) ambayo mfumo wake umeunganishwa na hospitali kubwa zote nchini ambapo mgonjwa ataendelea kupata huduma za kibingwa akiwa Songwe.
Kuhusu huduma Mollel amesema kulikuwa na daktari aliyemlipisha fedha 350,000 kinyume na utaratibu na akaondolewa na sasa uongozi uliopo unafanya kazi za huduma vizuri kwa kufuata miongozo iliyopo, mtoto chini ya miaka 5 na mama mjamzito hatakiwi kutozwa fedha za matibabu.
Kauli hiyo ya naibu waziri iliibua shangwe kwa wananchi hasa akina mama waliojitokeza kwenye uzinduzi huo, huku waziri mkuu akisisitiza madaktari kuongeza molali ya kuwahudumia wananchi kwani Rais Dr, Samia anatafuta fedha za miradi kazi iliyopo ni watumishi kuzitendea haki fedha hizo.
Leave a comment