WAZIRI mkuu Kassim Majaliwa ameeleza kushangazwa na idadi ya kesi mbili pekee kufikishwa mahakamani kati ya kesi 59 zinazohusu wanafunzi waliofanyiwa ukatili na kupewa ujauzito jambo ambalo linazidi kuzorotesha nia ya serikali kuwapatia elimu watoto wote wakiwamo wasichana.
Pia ameagiza maofisa elimu sekondari na msingi kwa kushirikiana na madiwani, wenyeviti na watendaji wa vijiji na kata kuhakikisha wanawasaka na kuwafikisha mahakamani ‘mafataki’ wanaoharibu ndoto ya wanafunzi. Anaripoti Ibrahim Yassin, Songwe…(endelea).
Majaliwa ametoa kauli hiyo leo Alhamisi alipotembelea Shule ya sekondari wasichana ya Ileje na kukagua ujenzi wa miundombinu ya shule hiyo.
“Ninataka kujua sababu ya kesi hizo za mafataki walioharibu ndoto za wanafunzi kutofika mahakamani,” amesema.
Amesema mkoa wa Songwe ni wa kwanza kitaifa kwa kuongoza kwa mimba za utotoni na wilaya ya Ileje ni ya kwanza kimkoa hivyo ni aibu kuwa na takwimu hizo.
Amewataka viongozi ngazi zote kushirikiana kutokomeza hali hiyo.
“Rais Samia anafanya kazi kubwa kutafuta fedha za maendeleo, miradi inajengwa lakini mnashindwa kusimamia mienendo ya watoto na vijana wasiowaaminifu wakiwemo waendesha bodaboda wamekuwa wakiwarubuni wanafunzi” amehoji Majaliwa.
Amesema serikali ni sikivu hivyo changamoto zilizotajwa zitafanyiwa kazi na kuhakikisha shule inakuwa na mazingira rafiki ya kusoma.
Akizungumza katika ziara hiyo, Mbunge wa Ileje ambaye pia ni Naibu Waziri wa Uchukuzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya amesema shule hiyo imeanza mwaka huu kwa kupokea wanafunzi 71 wa kidato cha kwanza waliofanya vizuri kwenye shule mbalimbali.
Naye Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Ileje, Nuru Kindamba amesema ujenzi wa shule hiyo ni mikakati ya serikali kumaliza mimba za utotoni.
Amesema shule hiyo bado inachangamoto ya mabweni ambayo yatasaidia wanafunzi kuishi maeneo ya shule.
Ameongeza kuwa changamoto iliyopo ni ujenzi wa uzio na miundombinu mengine itakayowezesha wanafunzi kusoma kwa usalama.
Leave a comment