SHIRIKA linaloshughulika na masuala ya msaada wa kisheria, Legal Services Facility (LSF), limetatua migogoro ya kifamilia 315, kupitia huduma yao ya mtandaoni waliyoanzisha – “Haki Yangu App”. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha … (endelea).
Hayo yameelezwa jana tarehe 7 Machi 2023 na Meneja wa Rasilimali na Mawasiliano LSF, Jane Matinde katika kongamano la kitaifa la wanawake, lililofanyika mkoani Arusha.
“Katika kuendana na ubunifu wa teknolojia ili kuwawezesha wanawake na wasichana kijamii na kiuchumi na kuhakikisha huduma za msaada wa kisheria na upatikanaji wa haki kwa wote, LSF tumezindua Haki Yangu App inayowezesha kupata elimu ya kisheria,” amesema Matinde na kuongeza:
“Kupata huduma za msaada wa kisheria, kutoa mafunzo maalumu kwa wasaidizi wa kisheria. Kupitia Haki Yangu App, kesi takribani 315 zikiwemo za unyanyasaji wa kijinsia, migogoro ya ardhi, mirathi, migogoro ya ndoa, matunzo kwa watoto zimeripotiwa na kufanyiwa kazi.”
Haki Yangu APP, ilizinduliwa Juni 2021, ambayo inawezesha wananchi hususan wanawake kuwasilisha malalamiko yao kwa ajili ya kupatiwa ufumbuzi wa kisheria.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Arumeru mkoani Arusha, Emmanuela Kaganda Mtatifikolo aliipongeza LSF kwa kudhamini kongamano hilo la wanawake, lililoandaliwa na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum.
Kongamano hilo lilikuwa na lengo la kujadili tafiti mbalimbali zilizofanyika katika masuala ya wanawake, ili kubaini hali halisi na kuweka mipango mikakati katika kushughulikia masuala ya wanawake katika nyanja ya kiuchumi, kijamii, na kisiaasa kwa ajili ya kukabiliana na vitendo vya ukatili wa kijinsia.
Amesema lengo la kujadili tafiti zilizofanyika kwenye masuala ya wanawake ni kuweka mipango ya kuyashughulikia.
Leave a comment