CHAMA cha Mapinduzi (CCM) kimefanya maamuzi magumu kwa kuwafuta uanachama viongozi wake waliopatikana na makosa ya maadili kinyume na katiba na kanuni za Uongozi na maadili ya chama hicho, anaandika Erasto Masalu.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Katibu wa NECm Itikadi na Uenezi wa CCM, Humphrey Polepole imesema mkutano wa Halmashauri Kuu ya Taifa imefikia maamuzi hayo kutokana na viongozi hao kukutwa na hatia.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa miongoni wa waliofukuzwa uanachama ni pamoja na mwanachama mkongwe na Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake (UWT) Sophia Simba huku Adam Kimbisa akisamehewa na Emmanuel Nchimbi akipewa onyo kali.
Watatu hao walionesha waziwazi kumuunga mkono aliyekuwa mgombea wa Urais kwa tiketi ya CCM, Edward Lowassa kabla ya kuhamia Chadema. Onyo kali alilopewa Nchimbi ina maana kuwa hatoruhusiwa kugombea nafasi yoyote kwa miaka minne.
Kufuatia maamuzi hayo, Sophia Simba amepoteza rasmi nafasi yake ya Ubunge wa Viti maalumu na Uenyekiti wa UWT kwani nafasi hizo zinahitaji mtu ambaye ni mwanachama wa chama aweze kuzishika.
Hivyo, CCM italazimika kupeleka jina lingine Tume ya Uchaguzi kuteua mbunge wa kuziba nafasi ya Sophia, huku nafasi yake ya Uenyekiti UWT ikisubiri uchaguzi baadae mwaka huu.
Wengine waliovuliwa uanachama ni Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Kinondoni Salum Kondo Madenge, Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Ilala, Assa Simba, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mara, Christopher Sanya, Mwenyekiti Mkoa wa Shinyanga Ernest Kwirasa, Mwenyekiti wa Mkoa wa Iringa, Nesta Msabatavunga, Mjumbe wa Halamshauri Kuu (NEC) ya CCM, Ali Sumaye, Mjumbe wa NEC Arumeru, Mathias Manga.
Wanachama weengine ni Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Longido, Makolo S. Laizer, Mwenyekiti wa CCM Arusha Mjini, Saileli Molleli, Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Gairo, Omary Hawadhi, Mwenyekiti wa CCM Babati, Ally Msuya, Mwenyekiti wa CCM Wilaya Bunda, Mjumbe wa NEC Gureta.
Waliopewa onyo kali kwa makosa mbalimbali ni Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Iringa Mjini, Ahmed Kiponza, Mjumbe wa NEC Mkoa wa Singida, Hassa Mzaha, Mwenyekiti wa UWT, Josephine Gezabulu, Mjumbe wa NEC Kilwa, Ali Mchumo na Mjumbe wa NEC Tunduru, Cheif Kalolo na Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Muleba, Muhaji Bushako.
Leave a comment