Wizara ya Afya imefuta matokeo yote ya mtihani wa usajili na leseni wa wauguzi na wakunga kwa watahiniwa 1,330 wa Stashahada baada ya kubainika kuvuja kwa mitihani hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Taarifa iliyotolewa leo tarehe 16 Januari 2024, Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Eiglibert Kayombo imesema matokeo hayo yamefutwa kwa mujibu wa Sheria ya Uuguzi na Ukunga ya Mwaka 2010, Kanuni ya mafunzo ya Mwaka 2010, Kifungu cha 22(3).
Amesema hatua hizi zimechukuliwa kwa lengo la kuhakikisha Baraza la Uuguzi na Ukunga Tanzania linathibitisha wataalam wenye sifa stahiki kulingana na taaluma zao kutoa huduma bora za matibabu kwa wagonjwa pamoja na kuzingatia usalama wa mteja anayetegemea kupata huduma za uuguzi na ukunga.
“Watahiniwa watapewa nafasi ya kufanya mtihani mwingine bila malipo yoyote na hawatahitajika kujisajili tena, mtihani utafanyika tarehe 16/02/2024, Dodoma. Taarifa zaidi kuhusu kurudia kwa mtihani huu zitatolewa na Baraza hivyo watahiniwa wote wanatakiwa kujiandaa na mtihani huo kwa kufuata taratibu kanuni na sheria,” amesema.
Amesema kwa upande wa watahiniwa wa ngazi za Astashahada na Shahada matokeo tayari yameshatoka na watahiniwa wamepata matokeo yao.
Hayo yamejiri baada tarehe 7 Septemba 2023, Baraza kuendesha mitihani ya usajili na leseni kwa Wauguzi na Wakunga 1,434 wa ngazi zote. Watahiniwa wa Astashahada walikuwa 44, Stashahada 1,330, Shahada 60.
Mitihani hiyo ilifanyika katika vituo vitatu katika mikoa ya Dar es Salaaam (DUCE); Mwanza (Mwanza University) pamoja na Dodoma (St. John University) na Wizara ya Afya ilipata taarifa za kuvuja kwa mtihani na kuchukua hatua za haraka kushirikiana na vyombo vya usalama kufanya uchunguzi ambapo ilithibitika kuwa ni ukweli mtihani ulivuja na kusambaa kwa watahiniwa wa Stashahada.
Aidha, Kayombo amesema mtuhumiwa aliyehusika katika uvujishaji wa mtihani huu tayari amebainika na kusimamishwa kazi huku taratibu kinidhamu na kisheria zinaendelea kutekelezwa.
Leave a comment