Friday , 29 September 2023
Home Habari Mchanganyiko Kisa cha Panya, Kuku, Mbuzi na Ng’ombe
Habari Mchanganyiko

Kisa cha Panya, Kuku, Mbuzi na Ng’ombe

Spread the love

NYUMBANI kwa mwanadamu uliwekwa mtego wa panya, lengo likiwa kumnasa panya. Anaandika Babu Jongo … (endelea).

Panya alipoona mtego akamuambia kuku amsaidie kuutegua, kuku akakataa, akasema hakutegwa yeye kwa hiyo haumuhusu.

Panya akamfuata mbuzi, akamwambia amsaidie kuutegua, mbuzi akasema haumuhusu kwa kuwa hakutegwa yeye.

Panya hakukata tamaa, akamfuata ng’ombe akamuomba amsaidie kuutegua mtego, akiamini nguvu za ng’ombe hata kama akiukanyaga tu mtego utavunjika.

Ng’ombe akacheka kwa dharau akasema haumuhusu, akamjibu panya apambane na hali yake.

Siku moja usiku kwenye mtego aliotegwa panya akanasa nyoka, baba mwenye nyukba aliposikia kishindo kwenye mtego akajua panya tayari ameshanasa.

Baba akamtuma kijana wake akamuue panya aliyenasa kwenye mtego, kijana alipokwenda kichwakichwa akagongwa na nyoka, sababu mtegoni alinasa nyoka na sio panya.

Kijana akafariki baada ya kugongwa na nyoka. Asubuhi kulipokucha watu wakaanza kujaa msibani.

Kwa kuwa watu walikuwa wengi kiasi, usiku akachinjwa kuku ili kuwapa watu kitoweo.

Siku ya pili ya mazishi akachinjwa ng’ombe ili kukidhi haja ya kitoweo na siku ya tatu ya kuondoa tanga akachinjwa mbuzi.

Kumbuka mtego alitegwa panya, alipowaambia kuku, mbuzi na ng’ombe wamsaidie kuutegua kutokana na uwezo wao wakakataa sababu hawakutegwa wao.

Lakini sasa wote hao waliojiona hawahusiki wamechinjwa na panya bado yuko hai.

Wakati raia wa kawaida wanatekwa na kupotezwa kuna watu walisema “shauri yao sisi hayatuhusu.”

Wakati Ben Saanane alipotekwa wengine wakapaza sauti za kutaka haki za raia zizingatiwe, lakini wengine wakasema watajuana wenyewe na Chadema wenzao.

Aliposhambuliwa Tundu Lissu, wapo waliosema amezidi kusema hovyo, wacha yamkute.

Akapotezwa mwandishi Azory Gwanda, wengine wakasema watajuana na waandishi wenzao waliozidi kufukunyua yasiyowahusu.

Akatekwa Roma Mkatoliki, upande mmoja wakapiga kelele aachiwe akiwa hai wengine wakasema afe kabisa, eti nani alimtuma aimbe siasa za kukosoa.

Watu wakaendelea kutekwa hasa upande wasiounga mkono chama kilichopanga Ikulu, na wale wanaojiona wenye chama na nchi wakafurahia.

Akakamatwa Manji, mwenyekiti wa klabu ya Yanga ya Dar es Salaam, akatupwa mahabusi, huyu ni mwanaccm kindakindaki, lakini baadhi ya mashabiki wa upande wa pili wakafurahia, wakatamani hata afilisiwe au afe kabisa, wengine bila kujali kuwa ni mwanaccm mwenzao.

Leo ametekwa Mohammed Dewj (MO), mwanaccm mwengine, mshirika wa karibu wa viongozi wengi serikalini na chamani.

Huyu ni mwanahisa kiongozi kwenye klabu ya Simba ya Dar es Salaam, ameshawahi kuwa mfadhili wa miaka mingi kwenye klabu hiyo.

Nuru inayowaka Simba kwa sasa inatokana na mkono wa MO, bahati mbaya tena yanatokea yaleyale.

Kuna mashabiki wa upande wa pili wanaomba MO asipatikane mpaka Ligi iishe au asipatikane kabisa akiwa hai.

Kutekwa kwa MO wao hakuwahusu, bado wanaamini wao wako salama.

Ni akili zilezile zilizotumiwa na kuku, mbuzi na ng’ombe, kuona mtego hawakutegewa wao.

Nani aliamini kama iko siku MO atatekwa kwenye ardhi ya Tanzania, tena asubuhi kweupe?

Nakuomba Mungu umsaidie MO apatikane akiwa hai na afya yake.

Lakini kipindi hiki ni muhimu kupata somo kwa wale waliokuwa wanajiona matukio haya hayatawagusa.

Ukiwa raia wa kawaida, mfuasi wa chama fulani, kiongozi wa chama, taasisi, serikali au hata dola – pinga, zuia upuuzi huu, jua nawe hauko salama hata kama unahusika na vitendo hivi vya utekaji.

BringBack MO Dewj & Others!

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari Mchanganyiko

Askari Polisi wa wanawake watakiwa kuchangamkia fursa za elimu

Spread the love  KAMISHNA wa Polisi Utawala Menejimenti ya rasilimali watu, CP...

Habari Mchanganyiko

Vijana 400 waguswa na programu ya “Learning for Life” ya SBL

Spread the love  PROGRAMU ya “Learning for Life” imetimiza dhamira ya Serengeti...

BiasharaHabari Mchanganyiko

Stamico yafungua fursa za kiuchumi kwa makundi maalumu

Spread the loveSHIRIKA la Madini la Taifa (STAMICO) limemwaga neema kwa watu...

BiasharaHabari Mchanganyiko

Maabara ya bilioni 5 upimaji madini yazinduliwa Geita, inapima kwa mionzi

Spread the loveZaidi ya Sh bilioni tano zimewekezwa katika kampuni ya MSALABS...

error: Content is protected !!