NAIBU Katibu Mkuu bara wa chama cha demokrasia na maendeleo (CHADEMA), Benson Kigaila, amesema mpaka sasa hamasa ya watanzania juu ya vyama vya upinzani hapa nchini bado ni kubwa licha ya kwamba wamekuwa kimya kutokana na sheria kandamizi. Anaripoti Apaikunda Mosha. TUDARCo … (endelea).
Ameyasema hayo katika mahojiano maalumu na Mwanahalisi Online na kuweka wazi mchakato wa maendeleo, mikakati na mafanikio ya chama cha demokrasia na maendeleo.
Akizungumzia maendeleo ya siasa hapa nchini Kigaila amesema, wananchi wamekuwa wakikandamizwa na kukosa haki zao za msingi kutokana na sheria mbaya zilizopo, kama kufungiwa kwa baadhi ya taasisi za Kiraia, serikali kusimamia shughuli za mahakama na kupandikizwa kwa migogoro inayoangamiza vyama vya Siasa hususani vya Upinzani.
Akizungumzia Katiba Mpya Kigaila amesema, suala la kupata katiba mpya ni jambo la muda mfupi na kudai kuwa gharama inayohitajika ni ndogo kwani tayari maoni ya watanzania yapo mezani kwenye rasimu ya Warioba.
Amebainisha kuwa kinachohitajika ni utashi wa kisiasa ili kuhakikisha kunakuwa na tume huru, wananchi wanapata haki zao, kuwepo na mifumo mizuri ya kiutawala na kutokomezwa kwa dhuluma.
Ameendelea kusema kuwa mpaka kufikia mwaka 2025 ana imani zoezi la kuwepo kwa katiba mpya litakuwa limekamilika na kama halitakamilika amedai uchaguzi hautafanyika.
“Hatutakubali kuona fedha za Watanzania zinatumika vibaya katika uchaguzi pasipokuwa na Katiba Mpya, maana Serikali imekuwa ikichukulia jambo hili kama ni dai la CHADEMA ilihali Rais mstaafu Jakaya Kikwete alikwisha unda tume ya katiba mpya ili kujenga taasisi imara za kusimamia na kuendesha utawala,” amesema Kigaila.
Hata hivyo Kigaila amewahakikishia Watanzania na Wanachama wa CHADEMA kuwa chama chao kinaendelea kujijenga na kuisuka taasisi hiyo ili kufanya chama kuwa imara na waweze kuhakikisha kuwa wana uwezo wa kulinda ushindi ambao wamepoteza kwa kuibiwa kura kila mara kwenye vituo vya kupigia kura.
Leave a comment