RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi amesema sheria mpya ya masuala ya habari ya Zanzibar inaandaliwa. Anaripoti Jabir Idrissa, Zanzibar … (endelea).
“Sheria ya Habari inaandaliwa na katika muda mfupi ujao itapelekwa kwa ajili ya kupitishwa na Baraza la Wawakilishi. Tutakuwa na sheria ambayo anayekataa kutoa taarifa serikalini atadhibitiwa,” alisema mbele ya Wahariri na Waandishi wa Habari waliofika Ikulu mjini hapa kushiriki mkutano wa kila mwezi na Rais wa Zanzibar.
Kauli hiyo aliitoa katika majibu yake ya swali aloulizwa na Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania – Tanzania Editors’ Forum (TEF), Deodatus Balile.
Mwenyekiti wa TEF ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Jamhuri Media Ltd, aliuliza kama sheria hiyo itakuja lini ili kuchangia wepesi wa upatikanaji wa taarifa serikalini. Alihoji tatizo la usiri wa kupita kiasi wa viongozi serikalini ambao unasaidia kuzorotesha utendaji makini wa vyombo vya habari nchini.
Katika maelezo aloyatoa kabla ya kuruhusu maswali, Rais Dk. Mwinyi alisema kuna ufichaji wa taarifa za kiutendaji serikalini kama ilivyooneshwa na ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) wa Zanzibar ya mwaka 2020/2021 alokabidhiwa wiki iliyopita.
Kumekuwa na jitiahada nyingi na nyakati mbalimbali kwa zaidi ya miaka kumi sasa za wadau wa sekta ya habari wakiwemo watetezi wa haki za binaadam kutaka serikali itunge sheria mpya ya huduma za habari kupisha sheria kongwe ya mwaka 1988 ambayo imekosa mazingira ya uwazi na uhuru kwa utafutaji, usambazaji na utoaji wa habari.
Leave a comment