ALIYEKUWA mgombea kiti cha Urais wa Kenya, Raila Odinga, pamoja na mgombea mwenza wake, Martha Karua, wamesema wanaheshimu maoni ya Mahakama ya Juu nchini humo ya kubariki matokeo yaliyompa ushindi mshindani wake, William Ruto, lakini hawakubaliani na uamuzi huo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Wanasiasa hao wametoa msimamo huo leo Jumatatu, tarehe 5 Septemba 2022, kupitia kurasa zao za Twitter, ikiwa ni muda mfupi tangu mahakama hiyo chini ya jopo la majaji lilioongozwa na Jaji Mkuu, Martha Koome, kutoa uamuzi huo.
“Siku zote tumesimama kwa utawala wa sheria na katiba, kuhusiana na hili tunaheshimu maoni ya mahakama ingawa hatukubaliani vikali na uamuzi wa leo,” ameandika Odinga katika ukurasa wake wa Twitter.
Odinga amedai mawakili wao walitoa ushahidi ya kwamba uchaguzi huo ulikuwa na dosari kwa kutoa hoja tisa, lakini kwa bahati mbaya majaji walizituplia mbali.
Amedai, licha ya uamuzi huo, bado wanaendelea na harakati za kuimarisha demokrasia ya Kenya na kwamba hivi karibuni wataainisha mipango yao ya kuendeleza mapambano dhidi ya uwazi, uwazi, uwajibikaji na demokrasia.
“Uamuzi huu si mwisho wa harakati zetu, kwa hakika unatutia moyo kuongeza juhudi zetu za kuivusha nchi hii hadi kufikia demokrasia yenye mafanikio ambapo kila Mkenya anaweza kupata haki yake,” ameandika Odinga.
Naye Karua, kupitia ukurasa wake wa Twitter ameandika “Mahakama imeongea, lakini sikubaliani na matokeo.”
Kwa mujibu wa uamuzi wa mahakama hiyo uliotolewa na jopo la majaji saba, mawakili wa Odinga wameshindwa kutoa ushahidi unaothibitisha matokeo ya uchaguzi huo yaliingiliwa.
Leave a comment