RAIS mstaafu wa Kenya, Uhuru Kenyatta, amesema nyumba ya mwanaye wa kiume imevamiwa. Anaripoti Mwandishi Wetu, kwa msaada wa BBC…(endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari, rais Kenyatta amesema, aliarifiwa na mtoto wake wa kiume, kwamba kuna watu wamefika nyumbani kwake na kujitambulisha kuwa ni maofisa wa polisi.
“…nimepigiwa simu na mtoto wangu wa kiume akaniambia kuwa wakati alipokuwa akitaka kutoka nyumbani kwake, aliambiwa kuna watu wanaodai kuwa ni kutoka DCI (Idara upelelezi ya makosa ya jinai), waliokuwa ndani ya gari lenye nambari za usajili za Sudan wanaotaka kuzungumza naye.’’
Rais Kenyatta amesema, alimwambia mwanaye asitoke nyumbani kwake na badala yake aliamua kwenda kwa mwanaye kuwaona watu hao.
“Nilitaka niende niwaulize ni nini wanatafuta kwa mwanangu,’’ alieleza.
Hata hivyo, Kenyatta anasema, alipofika alikuta tayari watu hao wameondoka.
Ameongeza: “Mnapaswa kunijia mimi, muache kuitisha familia yangu!’’…Msifikirie mnaweza kunitishia, mnaweza kutokubaliana nami …lakini sitaruhusu familia yangu kushambuliwa.”
Wiki hii mama yake Uhuru Kenyatta, Mke wa Rais wa kwanza wa Kenya, Mama Ngina Kenyatta, aliondolewa walinzi wake suala lililoibua hisia miongoni mwa Wakenya.
Akizungumzia suala hilo, Bw Kenyatta alisema, “usidhani unaweza kumtishia mwanamke mkongwe na wajukuu zake ili kunitisha mimi…Unafahamu nilipo saa 24, njoo nijie mimi.’’
Rais William Ruto amekuwa akimshutumu rais huyo mstaafu, kufadhili maandamano ya upinzani nchini humo yanayoongozwa na kinara wa upinzani, Raila Odinga.
Hizi ni chuki za kijinga viongozi wengi wa Afrika wanzifanya. Uhuru wa kuandamana unaruhusiwa kisheria kama sehemu ya kutolea dukuduku…siyo uchochezi.
Serikali nyingi za Afrika bado zinaendeshwa kikoloni. Sijui ni lini zitaacha na kujenga ukosoaji. “Kukosoa na kukosoana, ni silaha ya mapinduzi” JK Nyerere.