MAMLAKA ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), imewakaribisha Watanzania, kutoa maoni yao juu ya maboresho ya Kanuni za Maudhui Mtandaoni za mwaka 2018, ili ziwe rafiki kwa matumizi. Anaripoti Regina Mkonde, Morogoro … (endelea).
Wito huo umetolewa leo Jumanne tarehe 11 Mei 2021, Mkoani Morgoro na Mkuu wa Sheria wa TCRA, Dk. Phillip Filikunjombe, katika semina ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari wa mtandaoni, iliyoandaliwa na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC).
Dk.Filikunjombe amesema, lengo la mapitio ya kanuni hizo ni kuondoa kanuni ambazo zimekuwa zikipigiwa kelele na wadau mbalimbali hususan wa habari, kuwa zinakwaza upashanaji habari.
“Watu wa THRDC ni muhimu kuzingatia hili, TCRA imetangaza mapitio ya kanuni. Kulikuwa na nafasi watu watoe maoni kama unaona kuna mahali kanuni iondoshwe na baadhi ziboreshwe, andika maoni kifungu fulani kiondolewe.”
“Sema kifungu fulani kina shida, toa maoni yako, usijiangalie wewe unapotoa maoni, uangalie namna gani kanuni iboreshwe na wafikilie wengine kwa kundi kubwa ili kuona kanuni ziboreshweje. Tunataka kuweka mambo mazuri zaidi,” amesema Dk. Filikunjombe
Akizungumzia mabadiliko hayo, Dk. Filikunjombe amesema, kila nchi duniani, imekuwa ikitumia njia mbalimbali katika kuweka kanuni za matumizi ya maudhui mtandaoni na Tanzania ilikuwa miongoni mwa nchi hizo.
Mwaka 2020, Serikali iliona ije na kanuni za maudhui mtandaoni ikiwemo kuweka utaratibu wa vyombo vya habari mtandaoni, kupata leseni kwanza kabla ya kuanza kutoa huduma au adhabu kwa wakiukaji wa kanuni.
Amesema, lengo la TCRA kuweka kanuni hizo, sio kukandamiza au kubana watumiaji wa mtandaoni, bali lengo la kuratibu matumizi ya mitandao hiyo ili isitumike vibaya katika kukiuka haki za watu.
“Tanzania sio peke yake ina hangaika na uratibu wa ‘social media kwa Tanzania iliona walau tuwe na kanuni na sitaki kusema kama ni nzuri au mbaya lakini walau tuwe na utaratibu.”
“Tulikuwa na maoni kanuni hizi mbaya sana, sheria kandamizi, yawezekana kukawa na matumizi mabaya ya kanuni lakini nia ni njema walau tuwe na taratibu fulani,” amesema Dk. Filikunjombe.
Leave a comment