KAMATI ya Haki, Kinga, Maadili na Madaraka ya Bunge, imeshindwa kumhoji mbunge wa Ubungo (Chadema), Saed Kubenea, baada ya kuona hali yake ya kiafya imezorota, anaandika Dany Tibason.
Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Kampteni George Mkuchika, ameeleza wajumbe kuwa Kamati haiwezi kuendelea na mahojiano na Kubenea kutokana na afya yake kuyokuwa nzuri.
“Kubenea amefika hapa mbele ya Kamati kama ambavyo Spika wa Bunge alivyoagiza kuwa aletwe na polisi. Tumemuona na tumejiridhisha kuwa hatuwezi kuendelea na mahojiano,” ameeleza Mkuchika.
Amesema, “kutokana na hali hiyo, Kamati inaliagiza Bunge kumtibu Kubenea na baada ya hapo, tunaweza kuendelea na mahojiano yetu.”
Kubenea alifika mbele ya Kamati ya Haki, Kinga na Maadili leo asubuhi chini ya ulinzi wa polisi.
Alianza kushikiliwa kuanzia jana majira ya saa nne asubuhi baada ya kuripoti kwenye ofisi za Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Kinondoni.
Kwa sasa, Mhe. Kubenea amelazwa kwenye zahanati ya Bunge mjini Dodoma.
MwanaHALISI Online itaendelea kukujulisha kila hatua inayoendelea.
Leave a comment