IKIWA ni siku moja tangu kupinduliwa kwa Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi, James Mbatia, leo amekutana na zengwe jingine baada ya kuzuiwa kufanya mkutano na waandishi wa habari katika hotel ya Regency Park Mikocheni jijini Dar es Salaam kwa kile kilichoelezwa maagizo ya Mamlaka. Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).
Mbatia amezuiwa kufanya mkutano huo kwenye ukumbi wa Tanzanite ambao tayari baadhi ya wanahabari walifika kwenye kusubiri kuanza kwa mkutano huo uliopanga kufanyika saa saba kamili mchana.
Mwandishi wa Habari hizi amefika kwenye hoteli hiyo saa saba na dakika 8 na kuwakuta wanahabari wa vyombo vingine wakiwa mapokezi wakieleza kuwa wamezuiwa kupanda kwenye ukumbi wa mikutano na kwamba wahudumu wa hoteli hiyo walieleza kuwa shughuli hiyo imesitishwa.
Baada ya muda wa takribani dakika tano Mbatia aliyeambata na Angelina Mtahiwa Makamu Mwenyekiti wa Chama hicho Tanzania Bara, Anthony Komu Kaimu Katibu Mkuu , na Thomas Nguma mjumbe wa Bodi ya wadhamini ya chama hicho na wakili wake Ackson Chau walishuka chini na kutoka nje ambapo waandishi wa habari waliomba aseme alichokusudia kukizungumza nje ya hoteli hiyo ili kuepusha mgogoro.
https://youtu.be/tBglIw6iB48
Wakati huo huo alitokea Mwanamke mmoja ambaye hakujitambulisha jina lakini alitambuliwa kuwa ni mmoja wa viongozi wa hoteli hiyo na kumtaka Mbatia aondoke eneo hilo ili kuokoa kibarua chake.
Mtu huyu alionekana kupaisha sauti kana kwamba anagombana huku akiwataka wanahabari wasimrekodi na kusema “muondoke you still on my land’’ (mwondoke bado mpo eneo langu), huku akidai kuwa anawaita Polisi.
Baada ya Mzozo huo Mbatai na wenzake walitoka nje ya fensi ya hoteli hiyo na kufanya mazungumzo na waandishi waliohudhuria kwenye mkutano huo.
“Tumekuja hapa tumeomba tufanye mkutano kwenye ukumbi wa Regency Park lakini kwa bahati mbaya tumeambiwa kuwa uongozi umeshinikizwa na Mamlaka kuwa wasituruhusu kufanya mkutano hapa,” amesema Mbatia na kuongeza;
“Kabla mimi sijafika hapa na Wakili wangu Ackoson Chao tulipigiwa simu kuambiwa tusitishe mkutano huu kwa ajili ya usalama wangu na usalama wa Taifa nikambiwa nisitishe Mkutano huo kwa gharama yoyote ile.”
Leave a comment