KIONGOZI Mkuu wa chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Zuberi Kabwe amesema, chama chake, tayari kimekabidhi kwa Rais wa Zanzibar, Dk. Hussein Mwinyi, jina la mtu ambaye atakuwa Makamo wa Kwanza wa Rais Visiwani. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Zitto alisema, “tayari tumeshapendekeza jina kwa Rais wa Zanzibar la mtu ambaye atarithi majukumu ambayo Maalim Seif alikuwa anayafanya.
Aliongeza: “Bahati nzuri, Maalim Seif alikuwa ni Kiongozi. Alijua kuna siku Mwenyezi Mungu atamchukua, kwa sababu sisi sote lazima turejee kwa Mwenyezi Mungu kama tulivyoambiwa na mafunzo ya dini yetu na dini zote.
“Kwa hiyo, aliacha ametupa maelekezo ya nini kitokee iwapo atatangulia mbele ya haki.
“Namshukuru Mwenyezi Mungu kwamba viongozi wa chama wamefuata yale maelekezo yake kwa namna ambayo Kiongozi wetu alituelekeza. Sasa umebaki wajibu wa Rais wa Zanzibar wa kuyatekeleza hayo.”
Mchakato wa kumtafuta mrithi wa Maalim Seif Sharif Hamad, aliyekuwa Makamo wa Kwanza wa Rais Visiwani, ulianza Alhamisi iliyopita na kumalizika juzi Ijumaa, mjini Unguja.
Taarifa kutoka ndani ya chama hicho zinasema, Kamati ya Uongozi ACT-Wazalendo, imepitisha jina la mmoja wa viongozi watatu mashuhuri Visiwani, kumrithi kiongozi huyo.
Gazeti hili limefanikiwa kupata jina la kiongozi huyo, lakini kutokana na unyeti wa suala hilo, limeamua kulihifadhi kwa sasa.
Maalim Seif (77), alifariki dunia katika hospitali ya taifa ya Muhimbili, tarehe tarehe 17 Februari na akazikwa siku iliyofuata, kijijini kwake, Mtabwe, Pemba.
Mwamba huyo wa siasa nchini alifikwa na mauti baada ya kuwa hospitali kwa takribani wiki tatu, kufuatia kupata maambuziki ya virusi vya Corona.
Kwa mujibu wa Zitto, ambaye alikuwa akizungumza kwenye ibada ya hitima ya kumuombea kiongozi huyo, wanaamini kuwa huyo ambaye wamempendekeza kurithi nafasi ya Maalim Seif, “ataweza kusimamia maridhiano na haki za Wazanzibari kama ambavyo Maalim Seif mwenyewe alikuwa akifanya.”
Alisema, “tunawaomba muendelee kutuombea duwa ili tusitoke kwenye mstari, tuendelee kupigania demokrasia, haki na kuhakikisha kuwa nchi yetu inaendelea kuwa ya amani ili iweze kupata maendeleo ya watu.”
Leave a comment