CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimeonesha hofu ya kuchafuliwa kupitia uchunguzi unaofanywa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Tafukuru inaendesha uchunguzi kuhusu tuhuma za matumizi mabaya ya fedha zinazokikabili chama hicho. Tuhumza hizo zilitolewa na baadhi ya waliokuwa wabunge wa chama hicho ambayo walitangaza kuhama.
“Tuna mashaka sababu wigo wa uchunguzi hauoneshi ukomo wala kosa ambalo taasisi hiyo inachunguza. Tunaitaka Takukuru kufuata taratibu za kisheria katika uchunguzi wao ambao haujulikani utaisha lini na kuacha kutoa kauli za kisiasa,” amesema Mnyika.
Hofu hiyo imeelezwa tarehe 2 Julai 2020 na John Mnyika, Katibu Mkuu wa Chadema wakati akizungumza na wanahabari kuhusu sakata hilo.
Soma zaidi:-
Mpaka sasa Takukuru imehoji watu 60, wakiwemo viongozi na wanachama wa Chadema pamoja na kukabidhiwa nyaraka kadhaa zinazohusiana na fedha za michango ya wabunge wa chama hicho.
Mnyika amedai kuwa, uchunguzi huo unafanywa kisiasa, kwa lengo la kukichafua Chadema kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020, huku akisisitiza kwamba, hadi sasa Takukuru haijaweka wazi ukomo na aina ya tuhuma ambazo zinaikabili Chadema.
Wakati huo huo, Mnyika amedai kwamba, Chadema ina mashaka na uchunguzi huo wa Takukuru, baada ya taasisi hiyo kutaka nyaraka za chama hicho, ambazo hazihusiana na tuhuma husika.
“Wametuletea barua hazionyeshi ukomo wa uchunguzi, wanachungzua mambo mengine tofauti kabisa bila kueleza makosa yanayochunguzwa. Na wanahitaji nyaraka bila kueleza wanachunguza kwa masuala gani,” amedai Mnyika.
Baada ya tuhuma hizo dhidi ya Takukuru, MwanaHALISI ONLINE ilimtafuta kwa simu Brigedia Jenerali John Mbungo, Mkurugenzi Mkuu wa taasisi hiyo kwa ajili ya kupata ufafanuzi wake.
Akijibu tuhuma za taasisi yake kutumika kisiasa, Brigedia Mbungo amesema taasisi yake haifanyi kazi kisiasa, bali inaendeshwa kwa mujibu wa sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa.
Brigedia Mbungo amemtaka Mnyika kurejea Kifungu cha 7 (E) cha Sheria ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana, ambacho kinaeleza majukumu ya taasisi hiyo.
“Mwambie (Mnyika) asome hicho kifungu cha 7 cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, asiongee tu kama hajui sheria, kifungu cha saba kinasema kazi za Takukuru ni pamoja na kuchukua njia mahsusi kuzuia na kupambana na rushwa katika taasisi ya umma na taasisi binafsi,” amesema Brigedia Mbungo.
Brigedia Mbungo amesema, “Na kwa hiyo Takukuru itafanya yafuatayo, ukienda kipengele E inasema kuchunguza mambo yote ambayo yanatuhumiwa yamefanyika kuhusiana na ubadhirifu wa fedha.”
Kiongozi huyo wa Takukuru amesema taasisi hiyo haikukurupuka kufanya uchunguzi huo kama inavyodaiwa na Chadema, isipokuwa ilifanya hivyo baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa waliokuwa wanachama wa chama hicho.
“Taarifa hii ndio waliolalamika walisema kwamba kuna ubadhirifu wa fedha, ni wanachama wao ndio waliolalamika. Sasa sisi kila mtu anaweza akawa ni chanzo cha taarifa ambayo tunahitaji tuchunguze, walivyolalamika wao sisi tusingelala usingizi, ndio mmaana tunawachunguza,” amesema Brigedia Mbungo.
Kuhusu malalamiko ya Chadema kutakiwa kuipa Takukuru nyaraka zisizohusiana na tuhuma husika, Brigedia Mbungo amesema chama hicho kinapaswa kutekeleza kilivyoagizwa, ili wajue hatima yake, badala ya kupinga.
Leave a comment