Saturday , 27 April 2024
Home Gazeti Makala & Uchambuzi GGML mkombozi wa wahandisi wa kike katika sekta ya madini
Makala & Uchambuzi

GGML mkombozi wa wahandisi wa kike katika sekta ya madini

Spread the love

 

SI jambo rahisi kwa vijana wa kike kupenya na kufaulu vizuri katika taaluma mbalimbali ambazo zinashikwa na wanaume wengi zaidi hapa nchini Tanzania. Wanawake wengi huwa wanasita kuchagua kusoma fani hizo hususani uhandisi wa madini au jiolojia. Anaandika Mwandishi Wetu, Geita … (endelea).

Hali hii imechangia kuwepo kwa wahandisi wachache katika fani hiyo ya uhandisi ikilinganishwa na wanaume.

Kwa mujibu wa Bodi ya Usajili wa Wahandisi (ERB) mwaka 2018, iliweka wazi kuwa Tanzania ina uhaba wa wahandisi wa kike jambo linalorudisha nyuma maendeleo ya nchi.

Pia mwaka wa 2016, Taasisi ya Thomson Reuters Foundation ilitoa ripoti iliyoonesha kuwa licha ya wahandisi wa kike wa kwanza nchini  kuanza kuhitimu mwaka 1976, hadi kufikia mwaka 2009 ni asilimia nne tu ya wahandisi wote waliosajiliwa nchini Tanzania, ni wanawake.

Lakini chini ya Programu ya  Mafunzo maalumu kwa Wahandisi (SEAP), ambayo inakusudia kuwapa ujuzi na uzoefu kuwa wahandisi wa kitaalam katika uwanja unaotawaliwa na wanaume, mwanga umeanza kuonekana katika tasnia hiyo.

Programu hiyo, inayoendeshwa na Bodi ya Usajili wa Wahandisi ambacho ni chombo cha kitaalam cha Tanzania, kwa ufadhili wa serikali ya Norway, idadi ya wahandisi wanawake nchini Tanzania imeongezeka zaidi ya mara mbili tangu 2010.

Kuongezeka kwa idadi ya wahandisi  husuaani vijana wa kike kumesababisha mabadiliko ya haraka katika fani za kisayansi zinazoongozwa na wanaume kwani wahitimu wengi wa kike sasa wanapendezwa na taaluma za kisayansi licha ya kuvunjwa moyo na kukatishwa tamaa na wanaume ambao bado wanaamini kuwa wanawake hawawezi kukabiliana na changamoto katika ajira za aina hiyo kama vile sekta ya madini.

Hivi karibuni, Mwandishi wetu amezungumza na  Mhandisi Jesca Laswai ambaye ni Mhandisi wa Madini kitaaluma.

Jesca anafanya kazi kwa mkandarasi wa madini wa chini ya ardhi katika kampuni kubwa ya uchimbaji wa Madini mkoani Geita, yaani GGML.

Akizungumza kwa shauku na gazeti hili, anasema wanawake wengi hupendelea kusoma fani za aina hiyo lakini mazingira yanayowazunguka huwapa wakati mgumu kutimiza ndoto zao.

“Sidhani kama kuna taaluma maalum ya wanaume. Ikiwa ndivyo ilivyo, hatuwezi kuona wanawake wengi wenye talanta wakiweka rekodi za ulimwengu,” anaelezea Mhandisi Jesca.

Mhitimu huyo wa uhandisi wa madini kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam anasema wakati anasoma, alikuwa na shauku ya kutaka kuchunguza kwa kina tasnia ya madini.

“Haikuwa rahisi kwa sababu mara tu baada ya kuamua kufuata taaluma ya madini, watu wengi wa karibu walinishauri dhidi ya taaluma hii, asilimia kubwa walikuwa wakinikatisha tama na kuniambia napoteza wangu na hata kuhatarisha maisha ya baadaye ya familia yangu,” Jesca anaelezea.

Lakini Jesca anasema mambo yalibadilika baada ya kuchagua kazi hii, na sasa anafurahi sana kufanya kile anachofanya.

“Ninataka kuhimiza wanawake wengine wachanga na wahitimu wa vyuo vingine kuamini kuwa chochote kinawezekana katika sayari hii.

“Wanapaswa kuwa na shauku ya kutiumiza ndoto zao na kuchukua taaluma yoyote ikiwamo madini. Kazi hii ya madini inanihakikishia kupata mkate wangu wa kila siku hapa Geita. Ni kupitia shughuli hizi za uchimbaji wa madini hapa Nyankanga.

“Najua ni wasichana wachache wanaomaliza elimu ya sekondari nchini kutokana na umasikini uliokithiri, lakini pia wazazi wengi bado wanaendekeza tamaduni zilizopitwa na wakati kwamba wanawake wanatakiwa kutekeleza majukumu ya nyumbani.

“Lakini ikiwa wako shuleni, wasichana wamepata faraja kidogo ya kufuata masomo ya hisabati na sayansi, ambayo mara nyingi hufikiriwa kuwa uwanja wa wanafunzi wa kiume,” aelezea Jesca.

Katika miaka kumi ijayo, Jesca anajiona kama Mhandisi wa Madini aliyefanikiwa, ana matumaini kuwa atafikia kiwango hicho, sio tu kwa sababu anawezeshwa, lakini kwa sababu ana uwezo wa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kiwango kinachohitajika.

UTAJIRI WA MADINI TANZANIA

Tanzania ina utajiri wa maliasili, kama dhahabu, almasi, nikeli, urani, na gesi asilia. Pia Tanzani ni nyumba ya vito nadra zaidi duniani kama vile Tanzanite, ambayo hupatikana katika mkoa wa Manyara.

Licha ya rasilimali hizi za kipekee na uchumi unaostawi, Tanzania inashika nafasi ya 152 kati ya nchi 182 katika Kielelezo cha Maendeleo ya Binadamu, 134 kati ya nchi 185 zilizo katika mazingira mazuri ya biashara.

Hata hivyo, takriban asilimia 70 ya idadi ya watu wanaishi katika maeneo ya vijijini ambapo upatikanaji wa vifaa ni mdogo au haupo kabisa.

Kutokana na hali hiyo nchi inaendelea kukabiliwa na changamoto nyingi za kijamii na kiuchumi ambazo zimechangiwa zaidi na kiwango cha juu cha watu wasiojua kusoma na kuandika na kuacha masomo ya sayansi hali inayosababisha kuongezeka kwa ukosefu wa ajira.

Vivyo hivyo kwa upande wa wanawake wanakabiliwa na changamoto hii.

TAKWIMU ZA WAHANDISI ZINASEMAJE?

Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa bodi ya ERB, Mhandisi Ninatubu Lema anasema kwa sasa zaidi ya wahandisi 2,000 wanahitimu masomo katika vyuo vikuu nchini kila mwaka, lakini kati yao ni 800 tu wanaosajiliwa na ERB, huku zaidi ya wahandisi 1,200 wakitokomea kusikojulikana hali inayosababisha kuwapo kwa wahandisi hewa nchini.

Anasema idadi ya wahandisi waliosajiliwa nchini ni 21, 742 kati yao wanawake ni 2,153 ambao ni sawa na asilimia 10.

Anasema idadi ya wahandisi wanawake nchini imekuwa ikiongezeka na kwamba mwaka 2010  idadi yao walikuwa  96 tu  na hadi sasa imefikka 443, hiyo ni kwa jitihada ya nchi ya Norway ambao wamekuwa wakitoa ufadhili wa masomo kwa wahandisi wanawake.

Mhandisi Lema anasema licha ya kuwa na idadi hiyo, lakini  ni ndogo kulinganisha na mahitaji ya nchi inavyowahitaji wahandisi katika sekta ya ujenzi.

“Juhudi zinapaswa kuongezwa katika udahili wa wanafunzi katika vyuo vikuu, kwa maana idadi ya wanafunzi wa kihandisi wanaodahiliwa katika vyuo vikuu inapungua kila mwaka,” anasema mhandisi Lema.

Anasema changamoto inayoikabili taaluma ya uhandisi ni uhaba wa wahandisi, bajeti, rasilimali watu na fedha.

Hata hivyo, anasema Tanzania imekuwa ikikuza ustawi wa utoaji wa wanafunzi wengi zaidi ya asilimia 60 kulinganisha na nchi za Kenya na Rwanda.

Kutokana na changamoto hizo, anasema sera ya serikali ya awamu ya sita ya viwanda ina uhitaji mkubwa sana wa wahandisi ili taifa kufikia malengo na hivi sasa wameanzisha kampeni ya kuhamasisha wanafunzi waliyopo mashuleni kusoma masomo ya sayansi.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

BiasharaMakala & Uchambuzi

Kanda ya Ziwa yaonyesha NMB inavyosaidia afya ya mama na mtoto

Spread the loveMafanikio inayozidi kupata Tanzania katika kupunguza vifo vya mama na...

Habari za SiasaMakala & Uchambuzi

‘Mwanapekee’ wa Rais Samia: Atabadili nini Arusha?

Spread the loveMAPEMA wiki hii, baadhi ya viongozi walioapishwa na Rais Samia...

Habari MchanganyikoMakala & Uchambuzi

Kipunguni waihoji serikali, ziko wapi fedha za fidia?

Spread the loveWATU wanaodai kwamba serikali ya Chama Cha Mapinduzi ni sikivu,...

Habari za SiasaMakala & UchambuziTangulizi

Askofu Bagonza: Tusichonganishwe; tusichokozane na tusikufuru

Spread the loveJOTO la chaguzi linapanda kila siku hapa nchini. Upo umuhimu...

error: Content is protected !!