KEN Kandodo, Waziri wa Kazi wa Malawi na maofisa wengine wanne wa serikali ya nchi hiyo, wametimuliwa kazi kwa kukwapua fedha zilizotengwa kupambana na virusi vya corona (COVID-19). Inaripoti mitandao ya kimataifa … (endelea).
Maofisa hao wamefukuzwa kazi na Rais wa nchi hiyo, Lazarus Chakwera, baada ya kubaini ufisadi wa kwacha – fedha za Malawi – bilioni 6.2 (Dola za Marekani milioni 7.8) zilizotengwa kwa ajili ya kupambana na COVID-19.
Akitoa tamko la kuwafuta kazi maofisa hao, Rais Chakwera amesema, hakuna atakayesalimika na ukwapuaji wa fedha hizo huku akiarifu, tayari wahusika hao wapo kwenye vyombo vya sheria vya nchi hiyo.
Kiongozi huyo wa Malawi amesema, maofisa wengine waliohusika na ufisadi wa fedha hizo, watakamatwa katika siku zijazo huku akisisitiza, ripoti inaendelea kufanyiwa kazi.
“Siwezi kuwa na watu ndani ya baraza langu la mawaziri ambao wanatumia visivyo fedha zilizopangiwa kwa malengo tofauti,” amesema Rais Chakwera.
Waziri huyo ametuhumiwa kutumia vibaya kwacha 613,000 za Malawi zilizotengwa kwa ajili ya kupambana na corona.
Rais Chakwera amesema, licha ya waziri huyo kurejesha fedha, amesema hatua ya kutumia vibaya imejenga picha mbaya kwake na Taifa.
Leave a comment