KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Emanuel Nchimbi, amesema ndani ya chama chake kuna changamoto ya wagombea kukataa matokeo ya uchaguzi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es salaam…(endelea).
Dk. Nchimbi ametoa kauli hiyo leo tarehe 13 Aprili 2024, akizungumza na viongozi wa CCM Mkoa wa Katavi.
“Katika chama chetu tunayo changamoto moja, wanaoshinda mioyoni mwao wanakataa matokeo na walioshindwa mioyoni mwao wanakataa matokeo. Si wengi lakini wana madhara makubwa, mtu anachaguliwa kuwa mwenyekiti wa tawi lakini akishamaliza kuchaguliwa anaanza kutafuta nani wa kumuunga mkono aanze kupambana nao katika akili yake amejitengeneza yeye Mungu mtu na kila mtu amchague yeye,” amesema Dk. Nchimbi.
Dk. Nchimbi amesema tabia ya baadhi ya wana CCM kukataa matokeo inaleta taswira mbaya kwa vyama vingine vya siasa.
“Tukiwa chama kinachotawala kinachpaswa kutoa muelekeo na dira ya nchi, tunayofanya sisi ndani ya CCM ndiyo yanaakisiwa na vyama vingine. Mkiona vyama vingine vidogo vinaanza kukataa matokeo vinatuiga sisi tunavyokataa matokeo yetu wenyewe. Ndani mtu unapigwa mchana kweupe halafu unakataa matokeo,” amesema Dk. Nchimbi.
Katibu huyo wa CCM amewataka wanachama wa chama hicho kujenga desturi ya kuheshimu matokeo ya chaguzi.
“Tujue chama cha siasa madhubuti kinaongozwa na misingi ya demokrasia na demokrasia ya kweli kushiriki chaguzi huru na kukubali matokeo bila kusita. Mimi hapa nimegombea mara 28 na nimeshindwa mara nne na nimeshindwa vizuri sio kushindwa kidogo waswahili wanasema nimepigwa flat mara nne lakini nimegombea nikijua kwamba huu ni uchaguzi kuna kushinda na kushindwa,” amesema Dk. Nchimbi.
Leave a comment