Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es salaam (DAWASA), Kiula Kingu ametembelea na kukagua miundombinu ya maji iliyoathirika na mvua zinazoendelea kunyesha katika maeneo mbalimbali mkoani Dar es salaam na kuahidi maboresho yanafanyika usiku na mchana ili kurudisha huduma maeneo yaliyoathirika. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Kiula ametembelea eneo la Kimara Michungwani darajani ambapo uharibifu umetokea kwenye bomba la inchi 6, eneo la Bonyokwa Kijiweni uharibifu umetokea kwenye bomba la inchi 8, eneo la Mbezi Magufuli uharibifu umetokea kwenye bomba la inchi 6 na eneo la daraja la Gwajima – Mivumoni uharibifu umetokea kwenye bomba la inchi 6 na kupelekea wakazi wa maeneo hayo kukosa huduma ya maji.
Akizungumza baada ya ukaguzi huo, Kingu amesema athari iliyotokea kwenye miundombinu ni kubwa na kupelekea baadhi ya maeneo kukosa huduma, lakini DAWASA ipo kazini kuhakikisha huduma inaimarika.
“Ni kweli tumepata changamoto ya miundombinu ya maji lakini kwa jukumu tulilopewa ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma, hivyo niwaombe radhi wakazi wa Dar es salaam pia niwatoe hofu ya kuwa DAWASA tupo kazini kuhakikisha huduma inarejea na kila eneo lililoathirika linafikiwa na kufanyiwa maboresho” amesema Kingu
Vilevile, kwa upande wa miundombinu ya majitaka ameelezea kazi bado inaendelea ya kuzibua maeneo ambayo yalipata changamoto ya kuziba baada ya kuingiwa na mchanga pamoja na taka ngumu.
“Kwa upande wa miundombinu ya majitaka mafundi wetu wapo kazini ambapo wana vifaa vya kisasa wanaendelea na kazi ya kuzibua miundombinu, tunaendela kuwaomba wananchi kuwa wavumilivu DAWASA tumejipanga kuhakikisha hali inaimarika” amesema Kiula
Leave a comment