CHAMA cha Wananchi (CUF), kimeshauri marekebisho madogo ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977, ili kuzipa nguvu sheria za uchaguzi ambazo Serikali imepeleka miswada bungeni kwa ajili ya kuziboresha. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Kupitia taarifa yake kwa vyombo vya habari aliyoitoa jana Jumatatu, Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mahusiano na Umma CUF, Mhandisi Mohamed Ngulangwa alisema marekebisho hayo ya katiba yanapaswa kufanyika kabla ya chaguzi zijazo.
Mhandisi Ngulangwa alisema marekebisho ya katiba yatakayofanyika yanapaswa yaruhusu uwepo wa tume huru ya uchaguzi itakayosimamia Uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa 2024, Tanzania Bara na uchaguzi mkuu wa Jamhuri ya Muungano.
“TAMISEMI inatakiwa isisimamie uchaguzi wa serikali za mitaa, badala yake tume huru ya uchaguzi ifanye kazi hiyo,” alisema Mhandisi Ngulangwa.
Masuala mengine ambayo Mhandisi Ngulangwa alishauri yapatikane kupitia marekebisho hayo ni, ruhusa ya mgombea binafsi asiyedhaminiwa na chama cha siasa na rais atangazwe kashinda kama atapata zaidi ya asilimia 50 ya kura zote halali zilizopigwa.
“Ikiwa hakuna mgombea aliyepata zaidi ya asilimia 50 ya kura zote, uchaguzi utarudiwa na utakuwa na wagombea wawili walioongoza kwa kura nyingi. Pia, uchaguzi wa Rais uweze kuhojiwa mahakamani,” alisema Msemaji huyo wa CUF.
Pendekezo lingine alilosema Mhandisi Ngulangwa ni mawakala wa wagombea wa uchaguzi wasiwe na ulazima wa kula kiapo cha tume “muhimu wawe na barua ya uteuzi wa chama kinachowateua.”
“Watumishi wa Umma wanaogombea nafasi za kuchaguliwa wachukue likizo bila malipo. Wakishindwa uchaguzi waweze kurejea kwenye kazi zao,” alisema Mhandisi Ngulangwa na kuongeza:
“Asilimia 20 ya ruzuku ya serikali igawiwe sawa kwa vyama vyote vyenye usajili. Asilimia 80 igawiwe kwa uwiano wa wabunge na idadi ya kura za wabunge.”
Leave a comment