DAKTARI Dorothy Gwajima, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto nchini Tanzania amesema, matamko kuhusu magonjwa ya kuambukiza ikiwemo virusi vya corona (COVID-19), yametosha. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Amesema, matamko yaliyotolewa na Rais John Magufuli na pia Kasim Majaliwa, Waziri Mku yametoa mwanga mkubwa namna ya kujikinga na magonjwa hayo.
Dk. Gwajima ametoa kauli hiyo jana Alhamis tarehe 25 Februari 2021, wakati akitoa tamko la kuongeza kasi ya utekelezaji wa hatua za kujikinga na magonjwa hayo.
Amesema, matamko hayo yametosha kwa kuwapa ama kuwakumbusha wananchi nini wanapaswa kufanya katika kipindi hiki cha hekaheka za maambukizi.
Amesisitiza kwamba kila mmoja anapaswa kuwajibika na nafsi yake kwa kufuata miongozi ya afya iliyotolewa na wataalam.
“Matamko yameshatosha ya kuwapa mwanga wa nini wafanye, kinachopaswa kufanyika ni kila mmoja kuwajibika kwa nafasi yake,” amesema.
Ametaja mambo muhimu ya kuzingatia wakati wa kutekeleza hatua za kujikinga dhidi ya magonjwa hayo ni pamoja na kuondoa hofu.
Amekumbusha kwamba, kuna baadhi ya makundi yanayoathirika zaidi na magonjwa ya maambukizi ikiwa ni pamoja na wenye magonjwa sugu kama pumu, kisukari, shinikizo la juu la damu, figo. Amewataka kuchukua tahadhari zaidi.
“Jengeni tabia ya kuwahi katika vituo vya afya pale mnapoona dalili za kuumwa, pia jengeni tabia ya kupima afya angalau mara moja kwa mwaka hata kama humuumwi,” amesema.
Leave a comment