WAZIRI wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Stargomena Tax amesema Juni mwaka huu wizara hiyo kwa kushirikiana na wizara ya fedha inatarajia kukamilisha tathmini kujua kiasi gani cha bajeti kinahitaji ili kuliwezesha Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kuchukua wahitimu wote wa kidato cha nne na sita wenye sifa za kujiunga na jeshi hilo. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Dk. Tax amebainisha hayo leo Jumatatu bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Mafinga Mjini, Cosato Chumi (CCM).
Chumi alihoji iwapo Serikali ipo tayari kuiongezea Bajeti JKT ili kuwawezesha kuchukua wahitimu wote wa kidato cha Nne na cha Sita wenye sifa za kujiunga na JKT.
Akijibu swali hilo, Dk Tax amesema “Nimepokea ushauri wa Mbunge, tunaendelea kushirikiaa na wizara ya fedha kuongea bajeti kwa ajili ya makambi, kufanya tathmini kujua kiasi gani kinahitaji, tathmini inaendelea na tutatoa tarifa mwezi juni na baadae tutakuja na mpango mkakati utakaoainisha mahitaji yote,” amesema.
Aidha, amesema dhamira ya Serikali kutoa mafunzo kwa wahitimu wote ambao wana sifa ya kujiunga na mafunzo ya JKT kwa kujitolea, na kwa mujibu wa Sheria.
“Kwa sasa, vijana wote hawapati fursa ya kuhudhuria mafunzo hayo kutokana na ufinyu wa bajeti. Mpango uliopo ni kuijengea JKT uwezo ili iweze kuchukua vijana wengi zaidi wa kujitolea, na wahitimu wote wa kidato cha sita ambao wanastahili kujiunga na mafunzo ya JKT kwa mujibu wa Sheria, kwa kuongeza Bajeti ili kuboresha mafunzo na kuongeza idadi ya makambi.
“Wizara ya Ulinzi na JKT inaendelea kushirikiana na Wizara ya Fedha ili kuongeza miundombinu ya makambi, na bajeti ya kuendesha mafunzo ya JKT kadri uwezo wa Serikali utakavyoruhusu,” amesema.
Leave a comment