MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, amesema wamejipanga kuhakikisha Uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa 2024 na Uchaguzi Mkuu wa 2025, zinafanyika kwa amani mkoani humo. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Chalamila ametoa kauli hiyo leo tarehe 3 Aprili 2024, katika hafla ya uzinduzi wa Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi na mifumo ya usajili na malalamiko ya ukiukwaji wa misingi ya ulinzi wa taarifa binafsi, uliofanywa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, jijini Dar es Salaam.
Mkuu huyo wa Mkoa wa Dar es Salaam, amewataka wawekezaji wanaotaka kuwekeza mkoani humo kuja kuwekeza bila kuogopa chaguzi zijazo kwa kuwa wamejipanga kuhakikisha zitakuwa za amani.
“Nitoe rai mwaka huu tuna uchaguzi wa serikali za mitaa na mwakani uchaguzi mkuu, mara nyingi wawekezaji wanashindwa kuweka mitaji yao mingi kwenye uwekezaji katika sekta mbalimbali wakihofia vurugu ambazo zinakuwepo wakati wa uchaguzi mwaka huu,” amesema Chalamila na kuongeza:
“Nakuthibitishia mimi na wakuu wa wilaya tunashirikiana kwa kiasi cha kutosha kuhakikisha uchaguzi utakuwa imara, safi na wenye mitaji yenu msiogope kuja kuwekeza hasa katika mkoa wa Dar es Salaam, amani na utulivu ndiyo itakuwa kipaumbele chetu.”
Leave a comment