CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimeitaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kuwarejesha zaidi ya wagombea ubunge 30 na udiwani 600 walioondolewa kinyume na tarartibu za kanuni na sheria za uchaguzi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Benson Kigaila, Naibu Katibu Mkuu wa Chadema-Bara mbele ya waandishi wa habari leo tarehe 27 Agosti 2020, jijini Dar es Salaam akizungumzia shughuli ya uchukuaji na urejeshaji wa fomu za ubunge na udiwani, ameitaka NEC, kutatua mkwamo kwa maslahi ya Taifa.
“Tunaiomba Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kushughulikia haya, haiwezekani wagombea wetu pekee wa upinzani ndiyo wakosee kujaza fomu na wale wa CCM hawakosei, hii umewahi kuiona wapi,” amesema Kigaila na kuongeza:
“Tume bado ina nafasi ya kurekebisha makosa kama ili uchaguzi uweze kufanyika kwa amani kabisa, lakini kama tume haitatusikiliza na kutatua changamoto hizi ambazo zimejitokeza sisi Chadema hatutakubali,” amesema Kigaila.
Kigaila amesema, wagombea wao wameondolewa katika mazingira ya kutatanisha na wasimamizi wa uchaguzi, huku wakinyimwa fomu za kukata rufaa na wasimamizi wa uchaguzi jambo ambalo ni kinyume cha sheria.
Amesema, hali kama hiyo imejitokeza kwa wagombea udiwani zaidi ya 600 ambao wameondolewa, hivyo kuwafanya wagombea wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa udiwani na ubunge kuwa wagombea pekee wa maeneo haya.
Kigaila amesema, tayari wamewasilisha malalamiko ya maeneo yote Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ili iyashughulikie.
Leave a comment