CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimepanga kuvunja kauli ya Rais John Magufuli ya kukataza mikutano ya hadhara. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Kimeeleza kuwa, viongozi wake wanapanga ratiba ya kuzunguka nchini kufanya mikutano ya hadhara huku kikiweka wazi kuwa, kusimamisha mikutano hiyo hakukutokana katazo la Rais Magufuli.
“Kufanya mikutano ya hadhara siyo jinai na hata aliyezuia aliizuia kwa utashi, siyo kwa msukumo wa kisheria,” alisema Dk. Vincent Mashinji, Katibu Mkuu wa Chadema alipokutana na wanahabari Makao Makuu ya chama hicho, jijini Dar es Salaam jana.
Kwenye mkutano huo Dk. Mashinji amesema, kufanya mikutano ya hadhara ni uhuru wa kikatiba na kwamba sio jinai.
“…hata aliyezuia, aliamua hiyo kwa utashi, siyo kwa msukumo wa kisheria. Ni kweli, hata sisi tulikuwa na mambo ya ujenzi wa taasisi, kwa hiyo hatukuwa na uwezo wa kufanya vitu viwili kwa wakati mmoja,” alisema.
Katibu huyo wa Chadema alisema hayo wakati alipozungumzia maazimio yaliyofikiwa na kikao maalum cha Kamati Kuu ya chama hicho kilichofanyika tarehe 9 na 10 Februari mwaka huu.
Alisema, uamuzi huo umefikiwa baada ya chama hicho kukamilisha mipango yake ya ndani iliyohusu ujenzi wa chama hicho na kwamba, kinachofanyika kwa sasa ni upangaji ratiba itakayoongoza mahali na namna ya kufanya mikutano hiyo.
Dk. Mashinji pia alieleza kuwataka wapenda demokrasia duniani kupinga vikwazo vinavyoweka katika kukua na kuenea kwa demokrasia nchini.
Na kwamba, kuna watu wanaopinga kuwepo kwa mikutano ya hadhara kwa madai Chadema imekuwa ikitukana na kuwadhalilisha watu.
“Sisi huo muda mchafu hatuna, tuna sera zetu ambazo tunataka wananchi wazitambue. Tuna kazi kubwa ya kueneza sera zetu kuanzia mijini hadi vijijini, kwa hiyo hatuna muda mchafu wa kuongelea watu walioshindwa kutekeleza yale waliyoyaomba kikatiba,” alisema Dk. Mashinji na kuongeza;
“Tunawataka wapenda demokrasia wote duniani, kwanza kupinga hii mifumo isiyo ya kidemokrasia, kupinga kuingilia uhuru wa watu binafsi na uhuru wa taasisi zilizo huru,” alisema.
Jeshi la Polisi na Rais Magufuli wamekuwa wakikataza kufanyika kwa mikutano ya hadhara ya kisiasa kwa wanasiasa wanaotoka nje ya maeneo yao.
Rais Magufuli amekuwa akieleza kuwa, mikutano ya hadhara ya kisiasa haijakataliwa na kwamba, kilichopigwa marufuku ni mwanasiasa kwenye kuzungumza kwenye mkutano wa hadhara nje ya jimbo/eneo lake.
Leave a comment