RIPOTI ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) nchini Tanzania kwa mwaka 2020/2021 imebaini maduka ya dawa ya hospitali 15 za Rufaa na maalum yana dawa na vifaa tiba zenye thamani ya Sh.1.63 bilioni ambayo muda wake wa matumizi umeisha. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Ni ripoti inayoishia tarehe 30 Juni 2021 ambayo CAG Charles Kichere aliziwasilisha bungeni jijini Dodoma jana Jumanne 12 Aprili 2022.
Ripoti hiyo inaeleza, licha ya dawa hizo kuwemo hospitalini, uongozi wa hospitali hizo haujachukua hatua yoyote ya kuteketeza dawa hizo.
“Hali hii inatokana na kupokea dawa kutoka kwa wafadhili na Bohari Kuu ya Dawa zenye muda mfupi wa matumizi, kupungua kwa matumizi kutokana na kuanzishwa kwa dawa nyingine au mabadiliko ya mwongozo wa matumizi ya dawa zilizopo,” amesema CAG Kichere
Amesema alibaini kuwa 34% ya dawa zilizokwisha muda wake ni kutoka hospitali Maalumu ya Kibong’oto zenye thamani ya Sh. milioni 552 ikifuatiwa na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Katavi Sh. milioni 248, ikiwa ni 15%, hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Bukoba Sh. milioni 221 ikiwa ni 14%, wakati hospitali nyingine za rufaa zinawakilishwa na Sh. milioni 608, sawa ni 37% ya dawa zilizoisha muda wake wa matumizi.
CAG amezitaja baadhi ya hospitali hizo zenye dawa zilizoisha muda wake ni, Amana, Temeke na Mwananyamala za (Dar es Salaam), Mbeya, Mbeya-Kanda, Songea, Singida, Dodoma, Tanga, Shinyanga, Tumbi (Pwani), Mount Meru (Arusha) na Hospitali Maalum ya Kibong’oto.
Leave a comment