BUNGE limepitisha Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Huduma za Habari ya mwaka 2016 ambao umekuwa ukilalamikiwa na wadau mbalimbali wakitaka vifungu 21 vya sheria hiyo vibadilishwe. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Hata hivyo jana tarehe 13, jumla ya vifungu tisa pekee vimefanyiwa marekebisho katika Sheria hiyo ambayo ni moja ya sheria nane zilizopitishwa na Bunge katika muswada wa sheria mbalimbali iliowasilishwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Eliezer Feleshi.
Marekebisho ya sheria ya Huduma ya Habari yamekuja baada ya kilio cha muda mrefu tangu sheria hiyo ilipotungwa mwaka 2016, wakati wote wadau wamekuwa wapaza kelele sheria hiyo ifanyiwe marekebisho kwa kuwa inadumaza uhuru wa habari nchini.
Akitoa mchango wake kwenye muswada wa merekebisho wa sheria mbalimbali ikiwemo sheria ya huduma za habari wa mwaka 2023, Waziri wa Habari, Sayansi na Teknolojia, Nape Nnauye amesema wadau walipelekea mapendekezo katika vifungu 21 lakini kwenye mazungumzo walikubaliana vifungu nane vibaki kama vilivyo na vifungu tisa ndivyo vilivyopitiwa kwa makubaliano.
“Walileta mapendekezo 21, lakini wakati tunapitia tuliona marekebisho nane hayakuwa na ulazima hivyo tukayaacha kama yalivyo kwenye sheria ya awali lakini mengine tisa yalifanya marekebisho ikiwemo kuondoa jinai katika makosa ya kashfa (Difamation),” amesema Nape.
Amesema sheria hiyo imetoa nafasi kwa waandishi wa habari kuweka taaluma yao kama chombo kinachotambulika pamoja na kuwepo waandishi wenye sifa ili watoe habari zenye kuwatosheleza walaji.
Awali akiwasilisha hotuba yake bungeni, Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Eliezer Feleshi amesema kifungu cha 5 cha Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229 kinapendekeza kufanya marekebisho kwa lengo la kumwondolea Mkurugenzi wa Idara ya Habari jukumu la uratibu wa matangazo yote ya Serikali.
Pia marekebisho hayo yataiwezesha Serikali kuwa na uhuru wa kuchagua chombo cha habari itakachokitumia kwa ajili ya matangazo kwa kuzingatia nguvu ya ushindani katika soko.
“Inapendekeza kukifanyia marekebisho kifungu cha 38 kwa madhumuni ya kuongeza haki na uhuru wa maoni. Muswada unapendekeza marekebisho ya vifungu vya 50, 51, 53, 54, 55, 63 na 64 kwa madhumuni ya kuweka adhabu tahafifu kwa makosa yatokanayo na ukiukwaji wa sheria.
“Mapendekezo ya marekebisho ya vifungu hivyo yanakusudia kuondoa adhabu kwa wamiliki wa mitambo ya uchapishaji ambao katika hali ya kawaida hawana uwezo wa kudhibiti maudhui yanayochapishwa katika mitambo hiyo ya uchapishaji,” amesema.
Miongoni mwa adhabu zilizopunguzwa ni pamoja na eneo lililotaja kifungo cha kati ya miaka 5 hadi 10 ambapo sasa itakuwa miaka 2 hadi 5 wakati faini inashuka hadi Sh3 milioni na ukomo ni Sh10 milioni katika adhabu iliyokuwa ikienda hadi Sh20 milioni.
Muswada huo uliwasilishwa bungeni kwa mara ya kwanza Februari 10, 2023 na jana tarehe 13 Juni 2023 umejadiliwa na wabunge na kupitishwa pamoja na marekebisho katika baadhi ya vifungu vyake.
Leave a comment