BUNGE la Tanzania limesema wabunge 19 wa viti maalumu waliofukuzwa uanachama wa Chadema, wataendelea kutumikia mhimili huo hadi pale Mahakama Kuu, itakapotoa uamuzi dhidi ya kesi waliyofungua kupinga uamuzi wa kuvuliwa uanachama. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Akizungumza bungeni jijini Dodoma, leo Jumatatu, tarehe 16 Mei 2022, Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson amesema wabunge hao walimuandikia barua kumtaarifu kwamba wamefungua kesi katika Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam, tarehe 12 Mei mwaka huu.
Ikiwa ni siku moja tangu Baraza Kuu la Chadema, kutupilia mbali rufaa yao ya kupinga uamuzi wa kamati kuu ya chama hicho kuwafukuza uanachama kwa tuhuma za usaliti.
“Kwa mujibu wa katiba yetu, mamlaka yenye kauli ya mwisho ya utoaji haki ni mahakama. Hivyo, katika nchi zenye kuongozwa na misingi ya sheria na kuheshimiana kati ya mhimili mmoja na mwingine, Bunge haliwezi kuingilia mchakato wa mahakama, badala yake inalazimika kusbiri hadi hapo mahakama itakapotoa uamuzi wake kuhusu jambo hilo,” amesema Spika Tulia.
Spika Tulia amesema “Kwa mujibu wa katiba yetu na sheria tulizozitunga kama Bunge, kwa kuzingatia haya nalazimika kutotangaza nafasi viti maalumu 19 za Chadema ziko wazi, hadi pale mahakama itakapokamilisha uamuzi.”
Spika Tulia amesema, wabunge hao walifungua kesi kupinga uamuzi huo, wakidai ulichukuliwa kinyume na katiba ya Tanzania, kutozingatia haki ya msingi ya kuwasikiliza na kujitetea pamoja na mwenendo wa maamuzi uliofanyika ndani ya chama hicho haukuwa halali.
Kiongozi huyo wa mhimili wa Bunge, amesema kama kutakuwa na maswali yoyote juu ya suala hilo, mwenye kutoa ufafanuzi ni yeye.
Hata hivyo, Spika Tulia amesema, alipokea barua ya Chadema kuhusu uamuzi wake wa kuwafukuza uanachama wabunge hao kwa njia ya mkono, tarehe 13 Mei 2022, kutoka kwa Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho Bara, Benson Kigaila.
Leave a comment