WAZIRI wa Madini Dk. Doto Biteko amefurahishwa na namna Benki Kuu ya Tanzania (BOT) ilivyojipanga kufanya kazi kwa ukaribu na wachimbaji wadogo wadogo pamoja na wa kati hususani kwa hatua yao ya kutaka kuanza kununua dhahabu moja kwa moja kutoka kwa wachimbaji hao. Anaripoti Mwandishi Wetu, Geita … (endelea).
Biteko ametoa pongezi hizo Oktoba 3 mwaka huu katika ufunguzi wa Maonyesho ya Tano ya kitaifa ya Teknolojia ya Madini ambayo yanafanyika katika viwanja hivyo vya Bambambili mkoani humo.
“Nawashukuru sana Benki kuu kwa jitihada zenu ambazo mnazifanya ,Asanteni sana,” amesema Waziri Biteko.
Kwa upande wake Meneja Idara ya Mawasialiano kutoka Benki kuu ya Tanzania (BOT) Victoria Msina amesema kuwa benki hiyo imejipanga kuanza kununua dhahabu kutoka kwa wachimbaji wadogo na wakati mkoani Geita na hiyo itakuwa njia moja wapo ya kulinda akiba.
Amesema uwepo wao katika maonyesho ya madini mkoani humo ni njia moja wapo ya kuwaeleza umuhimu wa serikali kuwa na sera muhimu kwa ajili ya mstakabali mpana wa kukuza uchumi wa nchi.
Amesema wao kama BoT wanajua kuwa kuna wawekezaji wengi katika sekta ya madini hivyo wanapotembela kwenye banda lao wanawafundisha kuhusu kuwekeza katika amana ya serikali.
“Kuna umuhimu wa kutumia benki zetu na tunapotumia taasisi za fedha ziko salama na zinasimamiwa vizuri na Benki kuu ya Tanzania na kwasababu wachimbaji wadogo wadogo na wakati wanakuwa hawafahamu noti zetu kwahiyo tunawafundisha noti hizo ili waweze kuelewa alama za usalama zilizopo kwenye noti zetu.”
Leave a comment