VIONGOZI wa kijeshi waliochukua madaraka nchini Gabon wamemtangaza mkuu wa kitengo cha walinzi wa rais, Brice Clotaire Oligui Nguema, kama kiongozi wa mpito nchini humo. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa…(endelea).
Kwa mujibu wa taarifa za vyombo mbalimbali vya habari nchini humo, Brice Nguema ni binamu wa rais aliyeondolewa madarakani Ali Bongo.
Msemaji wa linalojulikana kama baraza la mpito, kupitia shirika la habari la serikali la Gabon 24, alimtangaza Nguema kama rais wa mpito jana Jumatano jioni.
Saa chache baada ya viongozi wa kijeshi kutwaa mamlaka, Rais Ali Bongo alionekana kwenye ukanda wa video akitoa wito wa usaidizi.
Bongo amewataka raia wa Gabon kupiga kelele na kueleza kuwa amezuiliwa kinyume cha sheria katika maakazi yake.
Kundi la maafisa wa ngazi ya juu jeshini wameiambia televisheni ya taifa kuwa Bongo anatuhumiwa kwa uhaini mkubwa.
Wakati hayo yanaarifiwa, mashirika ya kikanda na kimataifa yameonyesha wasiwasi wao juu ya kinachoendelea huko Gabon.
Ufaransa na Umoja wa Afrika umelaani mapinduzi hayo na kuhimiza suluhu ya amani kwa mzozo uliojitokeza baada ya uchaguzi katika nchi hiyo ya Afrika ya Kati.
Katika taarifa kwa vyombo vya habari, mwenyekiti wa kamisheni ya Umoja wa Afrika Moussa Faki ameyataja mapinduzi hayo ya kijeshi katika taifa hilo koloni la zamani la Ufaransa kama ukiukaji wa wazi wa sheria ikiwa ni pamoja na mkataba wa Afrika kuhusu uchaguzi, demokrasia na utawala.
Faki ametoa wito kwa jeshi la Gabon kuhakikisha usalama wa Ali Bongo, jamaa zake na baadhi ya maafisa waliokuwa wakimhudumia.
Leave a comment