NAIBU Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mhandisi Cyprian Luhemeja ametembelea na kukagua mradi wa maji Tarime – Rorya wenye lengo la kuboresha hali ya upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi wa Wilaya ya Rorya, Mji wa Tarime, Sirari pamoja na vijiji jirani. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Akizungumza mara baada ua kukagua mradi huo Mhandisi Luhemeja ametoa maagizo kwa mkandarasi anayetekeleza mradi huo Kampuni ya China Civil Engineering Construction Cooperation (CCECC) kukamilisha mradi kwa wakati kuwa hakutakua na muda wa nyongeza kumaliza kazi hiyo.
“Wananchi wanataka maji, hivyo namuagiza Mkandarasi kumaliza mradi huu ndani ya muda, ifikapo mwezi Aprili 2025 mkandarasi utakabidhi kazi hii, hakutakuwa na muda wowote wa nyongeza kutekeleza mradi huu,” ameeleza Mhandisi Luhemeja.
Kwa upande wake mratibu wa Mradi huo kutoka Wizara ya Maji, Mhandisi Joel Rugemalila ameeleza kuwa kazi inaenda vizuri na watahakikisha wanamsimamia mkandarasi ili akamilishe mradi kwa wakati.
“Mkataba huu ni wa miezi 30 utakamilika kwa wakati, Wilaya ya Tarime, Rorya na Mji wa Sirari unaenda kuondokana na changamoto ya upatikanaji Majisafi,” ameeleza Mhandisi Rugemalila.
Mradi wa maji Tarime-Rorya unahusisha ujenzi wa chanzo chenye uwezo wa kuzalisha maji lita milioni 29 kwa siku, ujenzi wa Bomba kuu kwa umbali wa Km 90, ujenzi wa matenki matatu yenye ujazo wa Lita milioni 6 Rorya, milioni 1 Sirari, na lita milioni 3 Tarime, ulazaji wa mtandao wa maji kwa umbali wa Km 20 pamoja na ujenzi wa vituo vitatu vya kusukuma maji.
Kukamilika kwa mradi huu kutanufaisha jumla ya wakazi 933,816 katika vijiji 32 vya Wilaya ya Rorya pamoja na mitaa 81 ya mji wa Tarime.
Aidha, mradi huu utaongeza huduma ya upatikanaji majisafi na salama wilayani Rorya kutoka 53.4 inayopatikana sasa hadi kufikia asilimia 90. Kwa upande wa halmashauri ya mji wa Tarime, huduma itapanda kutoka asilimia 63.4 hadi zaidi ya 95.
Leave a comment