BEI za mafuta zitakazotumika mwezi Februari 2024, zimeshuka ambapo kwa Jiji la Dar es Salaam, imeshuka kwa wastani wa Sh. 33 kwa kila lita ya Petroli , huku dizeli ikishuka kwa Sh. 49. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo tarehe 7 Februari 2024 na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji nchini (EWURA), Dk. James Mwainyekule, akitangaza bei kikomo za bidhaa ya mafuta ya petrol kwa mwezi huu.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, bei ya Petroli itakayotumika jijini Dar es Salaam, imeshuka kutoka Sh. 3,084 iliyotumika Januari hadi kufikia Sh. 3,051 itakayotumika Februari. Upande wa Dizeli imeshuka kutoka Sh. 3,078 (Januari) hadi kufikia Sh. 3,029 (Februari).
Upande wa Tanga, bei ya petrol imebaki palepale ya Sh. 3,064 iliyotumika Januari, wakati dizeli ikishuka kwa Sh. 23 kutoka Sh. 3,219 iliyotumika Januari hadi kufikia Sh. 3,196 itakayotumika mwezi huu.
Taarifa hiyo imeonesha pia viwango vya bei katika mikoa mingine ambapo kuna baadhi yake bei ya petroili haijapanda wala kushuka wakati dizeli ikishuka kama mkoa wa Arusha.
Mbali na petroli na dizeli, taarifa hiyo imeonyesha bei ya mafuta ya taa kwa Februari imepungua pia.
Sababu za kushuka kwa bei hizo zimetajwa kuwa ni kupungua kwa bei zake katika soko la dunia kwa wastani wa asilimia 10.66 kwa Petroli na asilimia 11.20 kwa dizeli na asilimia 5.82 kwa mafuta ya taa.
“Pia kupungua kwa bei za mafuta kumetokana na kushuka kwa gharama za uagizaji wa mafuta kwa Bandari ya Dar es Salaam kwa wastani (weighted average) wa asilimia 9.69 kwa dizeli na asilimia 1.82 kwa mafuta ya taa. Vivo hivyo, gharama za uagizaji wa mafuta ya petroli na dizeli kwa Bandari za Tanga na Mtwara zimepungua kwa wastani (weighted average) wa asilimia 0.69 na 11.93, mtawalia,” imesema taarifa hiyo.
Leave a comment