BARAZA la Wanawake wa Chama cha Demokarasia na Maendeleo (Bawacha), nchini Tanzania, limesitisha kongamano la ‘Siku ya Wanawake Duniani’ kitaifa, lililopangwa kufanyika mkoani Iringa, 8 Machi 2021. Anaripoti Matrida Peter, Dar es Salaam … (endelea).
Sababu zilizosababisha kuahirishwa kwa kongamano hilo, ni kuzuia maambukizi ya virusi vya corona (COVID-19).
Uamuzi wa kuahirisha, ulifikiwa jana Jumatatu tarehe 1 Machi 2021, katika kikao cha kamati ya utendaji ya Bawacha, iliyokutana kwa njia ya mtandao.
“…imefikia uamuzi huo, ikiwa ni jitihada mojawapo ya kuzuia maambukizi ya virusi vya corona, vinavyosababisha ugonjwa wa COVID-19 (matatizo kwenye mfumo wa hewa wa binadamu), yanayosababisha vifo kwa wapendwa wetu,” amesema Sharifa Suleiman, makamu wa Bawacha-Zanzibar, kupitia taarifa yake kwa umma
Amesema, zaidi ya wanawake 3,000, kutoka mikoa mbalimbali nchini, walikuwa wamethibitisha kushiriki hivyo, itakuwa vigumu kuepuka msongamano, kutokana na tukio lenyewe.
Sharifa amesema, hali itakaporuhusu mkusanyiko mkubwa kama huo, Bawacha itatangaza mahali na tarehe rasmi ya kungamano jingine maalum ambalo, litakutanisha wanawake wote.
Leave a comment