MAMLAKA ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), imetengeneza kanuni ndogo zitakazoratibu bei za vifurushi vya mitandao ya simu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Ni baada ya maoni ya wateja yaliyojikita katika kulalamikia huduma hiyo, sambamba na kutoelewa namna vifurushi hivyo vinavyoisha.
James Kilaba, Mkurugenzi Mkuu wa TCRA ametoa kauli hiyo leo Jumanne tarehe 2 Machi 2021, akisisitiza taasisi hiyo itaratibu utoaji wa huduma hiyo.
Kilaba amesema, utekelezaji wa kanuni hizo unatarajia kuanza tarehe 2 Aprili 2021.
Miongoni mwa yaliyomo katika kanuni hizo ni pamoja na huduma zote za vifurushi, lazima zipate vibali vya TCRA na vitadumu kwa siku 90, kabla ya kufanyika kwa mabadiliko mengine, tofauti na sasa, vifurishi vinabadilishwa ghafla.
Na kwamba, pamoja na kutoa vibali lakini itakuwa na mamlaka ya kutoa mwongozo wa bei.
Pia kanuni hizo zinaelekeza, kwamba mtoa huduma atatakiwa kutoa taarifa pale matumizi ya kifurushi husika yatakapofika asilimia 75, na pale kifurushi kitakapokwisha.
“Mtoa huduma, atahakikisha bei za vifurushi zinazingatia bei husika ya chini na ya juu zilizowekwa na mamlaka na atatumia lugha rahisi na vigezo na masharti yaliyo wazi kuhusu vifurushi vinavyotolewa,” amesema
Kilaba amesema “mtoa huduma, ataweka program rununu (Mobile App) ya kumwezesha mtumiaji wa huduma mwenye simu janja kufuatilia matumizi yake ya data kwa kupakua program rununu hiyo ya mtoa huduma.”
Leave a comment