KLABU ya Simba itaondoka nchini leo kuelekea Khartoum, Sudan kuwavaa El Merreikh kwenye mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika utakaopigwa tarehe 6 Machi 2021, huku jina la mchezaji Bernard Morrison likikosekana kwenye orodha ya wachezaji watakaosafiri. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Simba itaondoka na wachezaji 25, kupitia Uwanja wa ndege wa kimataifa wa Julius Nyerere majira ya saa 10:45 jioni na Shirika la Ndege la Ethiopia na watawasili nchini Sudan kesho mchana.
Morrison ameachwa kutokana na kuwa majeruhi baada ya kuumia katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Biashara United uliopigwa kwenye Uwanja wa Karume, Mara.
Simba inaenda kucheza mchezo huo huku ikiwa imefanya vizuri kwenye michezo miwili ya awali na kujiokotea pointi sita baada ya kuwafunga AS Vita na Al Ahly.
Mpaka sasa kwenye kundi A, Simba wanashikilia nafasi ya kwanza wakiwa na pointi 6 baada ya kucheza michezo miwili, huku nafasi ya pili ikishikwa na AS Vita akiwa na pointi tatu sawa na Al Ahly nafasi ya mwisho inashikwa na El Merreikh ambayo haina pointi.
Leave a comment