BARAZA la Vijana la Chama cha Chadema (BAVICHA), limewataka viongozi wake wa mikoa ambao ni waoga, wakae pembeni ifikapo 2023 maana mwaka huo utakuwa mwaka wa harakati endapo maridhiano yanayofanywa na Serikali pamoja na vyama vya upinzani hayatazaa matunda.Anaripoti Mwandishi Wetu, Shinyanga…(endelea).
Wito huo umetolewa jana tarehe 30 Desemba 2022 na Mwenyekiti wa BAVICHA Taifa, John Pambalu, akizungumza na wanachama wa Chadema mkoani Shinyanga.
“2023 utakuwa ni mwaka wa movement kubwa ya vijana, 2023 chama kipo kwenye tathmini ya hali ya maridhiano watakapoona ama watakapotoa muelekeo kwamba hayajaleta matunda kama noma na iwe noma, vijana wa hovyo mtafute chama cha kwenda sio Chadema,” alisema Pambalu na kuongeza:
“Kama kuna mwenyekiti wa BAVICHA muoga apishe, aseme bwana imekwisha na tutamshukuru tutamuona muungwana kuliko kusema saa 12 tunakutana sehemu fulani ili tuanze maandamano kabla hajajiandaa halafu saa 12 mnajikuta hampo. Bora waondoke tubaki wanaume wa kazi tuikomboe nchi hii.”
Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan, iliyoingia madarakani Machi 2021, imechukua jitihada mbalimbali za kufanya mazungumzo na viongozi wa vyama vya siasa vya upinzani kwa ajili ya kutafuta maridhiano yenye lengo la kuboresha demokrasia ya vyama vingi.
Miongoni mwa maridhiano hayo ni namna ya kuimarisha uhuru wa vyama vya siasa kufanya siasa, uondolewaji zuio la mikutano ya hadhara, upatikanaji tume huru ya uchaguzi, katiba mpya na hata marekebisho ya sheria zinazosimamia vyama hivyo.
Leave a comment