WAZIRI wa Kilimo, Hussein Bashe, amewahakikishia wananchi kuwa hakutakuwa na uhaba wa mbolea kutokana na Serikali kutoa zuruku na kushusha bei ambazo hivi sasa zipo juu. Anaripoti Apaikunda Mosha, TUDARCo … (endelea).
Mbali na hilo amewahakikishia wakulima kuwa bei za mbolea zitakuwa ni moja kwa nchi nzima bila kujali umbali wa mkoa kutoka bandarini ambako ndiko mbolea hushushwa kutoka nje.
Bashe ameyasema hayo leo Alhamisi tarehe 11 Agosti wakati akiwahutubia wananchi wa Ludewa mkoa wa Njombe akiwa katika msafara wa Rais Samia Suluhu Hassan kuelekea mkoani Iringa ambako ameanza ziara yake.
“Kuanzia tarehe 15 mwezi huu wakulima wote nchi nzima wataanza kununua mbolea kwa bei elekezi aliyotoa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu, mawakala wa nchi nzima watauza bei ya DPA kutoka bei ya Sh 130,000 na Sh. 140,000 mpaka Sh 70,000 kwa mikoa yote.
Amesema UREA sasa itanunuliwa Sh. 70,000, KAN ambayo itanunuliwa Sh. 60,000, SK Sh. 50,00, NPK na YARAMIA zikinunuliwa kwa Sh 70,000.
Amefafanua zaidi kuwa mgawanyo huo wa bei utajumuisha na faida zao kwani serikali itachukua asilimia 50 na wakulima watalipa asilimia 50.
Waziri Bashe amewaomba wakulima wote kwenda kujisajili kwenye uongozi wa serikali zao za vijiji kwa kutumia vitambulisho au namba ya NIDA na namba ya simu, “pia watachukua jina, ukubwa wa shamba, aina ya mazao, picha na alama ya dole gumba, na watapatiwa namba ya siri.”
Aidha amewataka wananchi kuwa waaminifu kwani hata watakapoenda kununua mbolea kama watakuwa hawajasajiliwa wawe wawazi ili kusaidia kujua idadi itakayokuwa imeuzwa na mahali pamoja na mkulima aliyenunua kwani wakala anapouza atakuwa anaandika jina la aliyenunua.
“Unaponunua mbolea angalia imebandikwa stika, hii itasaidia kuzuia watu ambao walikuwa wanafaidika kabla ruzuku hazijamfikia mkulima,” amesema Bashe.
Leave a comment