KIONGOZI wa waangalizi wa Uchaguzi Mkuu wa Kenya kutoka Jumuiya ya Afrika Mashariki, Rais mstaafu wa Tanzania, Jakaya Kikwete ametoa wito kwa wagombea ambao hawatakubaliana na matokeo ya uchaguzi huo watumie njia za kisheria kwenda mahakamani badala ya kutumia njia nyingine zisizo sahihi. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Pia Kikwete ambaye anaongoza timu ya watu 43 kutoka EAC amesema uchaguzi huo umefanyika umefanyika kwa amani, utulivu na uwazi kutokana na maandalizi yaliyofanywa na Taifa hilo pamoja na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC).
Itakumbukwa kuwa mwaka 2017, Mahakama ya Juu iliyafuta matokeo ya kura ya urais ya uchaguzi huo baada ya kukubaliana na hoja za mgombea urais Raila Odinga kwamba kulikuwa na kasoro kwenye ukusanyaji na usafirishaji wa matokeo hayo hadi Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) ya Kenya.
Kikwete ametoa kauli hiyo, leo tarehe 11 Agosti, 2022 wakati akitoa ripoti ya awali kuhusu mchakato wa uchaguzi mkuu wa Kenya ambao umefanyika tarehe 9 Agosti mwaka huu.
Ripoti hiyo ya Kikwete pia inahusu hali ilivyo sasa wakati matokeo yakiendelea kutangazwa katika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo.
“Tunawasihi muendeleze amani na utulivu baada ya matokeo kutangazwa, kama mtu atakuwa na pingamizi kuna mwanya wa kisheria hivyo wachukue mkondo huo” amesema.
Amesema anaamini matokeo yatakayotangazwa na IEBC ndiyo yatakayoakisi kilichofanyika katika vituo mbalimbali na ndicho Wakenya walichokitaka.
Aidha, akizungumzia kasoro walizozibaini katika uchaguzi huo mosi amesema licha ya vituo vingi vya kupigia kura kufunguliwa mapema, baadhi vilichelewa kufunguliwa bila sababu za msingi.
Pia amesema baadhi ya mashine za utambuzi wapiga kura zilikuwa na kasoro katika baadhi ya vituo, hivyo kusababisha baadhi ya watu kuchelewa au kushindwa kupigwa kura kutokana na muda wa kupiga kura kuisha saa 11 licha ya kasoro zilizojitokeza.
Amesema pamoja na mambo mengine wamebaini vijana wengi wamelalamikia vyama vya siasa kutowapa fursa ya kugombea nafasi mbalimbali katika uchaguzi huo jambo ambalo linapaswa kuangaliwa kwa umakini katika chaguzi zijazo.
Ameongeza kuwa kasoro zilizojitokeza katika uchaguzi huo, zinatakiwa kutiliwa maanani na tume hiyo ya uchaguzi ili kudhibiti kasoro hizo zisijitokeze tena.
“Pia tunawapongeza tume kwa kuajiri vijana wengi tena wa kike kusimamia uchaguzi huu kwa uweledi mkubwa, inaonesha wamepewa mafunzo ya kutosha jambo ambalo limeongeza ufanisi katika kazi hii,” amesema.
Mbona Tanzania wanaoshindwa uchaguzi wa urais hawaruhusiwi kwenda mahakamanai?