MWANAUME mwenye umri wa miaka 42 amewapiga risasi watu saba wa familia yake kabla ya kujiua katika jimbo la Utah nchini Marekani baada ya mkewe kuwasilisha maombi ya talaka, polisi walisema. BBC imeripoti … (endelea).
Familia ya wanane ilipatikana imekufa ndani ya nyumba ya mashambani katika Jiji la Enoch Jumatano usiku wakati wa ukaguzi katika boma lao.
Polisi walisema waliouawa ni pamoja na mke wa mwanaume huyo, watoto wake watano na mama mkwe wake.
Meneja wa jiji Rob Dotson alisema mji huo wenye watu wapatao 8,000 ulikuwa katika mshtuko.
Katika mkutano na wanahabari siku ya Alhamisi, maafisa wa jiji walisema mfanyabiashara wa bima mwenye umri wa miaka 42 Michael Haight alimfyatulia risasi mke wake Tausha mwenye umri wa miaka 40, mama mkwe wake Gail Earl mwenye umri wa miaka 78 na watoto wake watano na kisha akajiua
Watoto hao watano ambao hawakutajwa majina yao ni pamoja na wasichana watatu, wenye umri wa miaka 17, 12 na 7, na wavulana wawili, 7 na 4.
Meneja wa Enoch City Rob Dotson alisema miili yao iligunduliwa na polisi mwendo wa 16:00 saa za ndani (23:00GMT) siku ya Jumatano, baada ya mtu kuripoti kwamba mke alikosa miadi iliyopangwa, na kusababisha ukaguzi kwenye nyumba ya familia.
Dotson alisema kila mmoja wa waathiriwa alionekana kuwa na jeraha la risasi.
Maafisa pia walithibitisha kwamba mke alikuwa amewasilisha ombi la talaka tarehe 21 Desemba.
“Tausha alikuwa mtu mkarimu na hakuwahi kusema lolote baya kuhusu mtu yeyote,” Tina Brown, rafiki wa familia hiyo, aliambia KSTU-TV.
Maafisa wa jiji, akiwemo meya Jeffrey Chestnut, walionekana kuwa huzuni walipotoa taarifa zao za hivi punde kwa vyombo vya habari.
“Si mara nyingi sana jambo kama hili hutokea karibu na nyumbani,” Chestnut alisema, akiongeza kuwa familia ya Haight walikuwa majirani zake.
Leave a comment