BEKI matata kutoka Ujerumani, Antonio Rudiger amekamilisha uhamisho wake kutoka Chelsea kuelekea Real Madrid.
Tarehe 2 Juni, 2022 The Blues walimuaga Rudiger baada ya kuwa nao kwa kipindi cha miaka mitano. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Rudiger (29), amejiunga na Real Madrid bila ada yoyote kwa kuwa mkataba wake na Chelsea ulikuwa unaelekea ukingoni.
“Ameondoka akiwa ametoa mchango mkubwa katika mafanikio yetu katika misimu ya hivi karibuni.
“Rudiger alinyanyua Kombe la FA, Ligi ya Mabingwa, Ligi ya Europa, UEFA Super Cup na Kombe la Dunia la Vilabu la FIFA akiwa na Chelsea huku akicheza jukumu muhimu katika ushindi huo wote katika moyo wa ulinzi wetu,” taarifa ya Chelsea ilieleza.
Beki huyo ambaye alijiunga na Chelsea mwaka wa 2017 anaondoka baada ya kuwakilisha klabu hiyo katika mechi 203 na kuifungia jumla ya mabao 12.
The Blues wamesema Rudiger hakuwa mchezaji mahiri tu bali pia kiongozi shupavu kwa timu hiyo.
Rudiger amesema kwamba yupo tayari kwa changamoto mpya nchini Uhispania akiwa na klabu yake mpya ya Madrid.
“Ninajivunia kutangaza kuwa nitakuwa najiunga na Real Madrid. Nina furaha kubwa kwa changamoto zilizo mbele na siwezi kusubiri kucheza mechi zangu za kwanza kwa klabu hii kubwa,” Rudiger alisema kupitia Twitter.
Real Madrid imemkaribisha beki huyo kupitia kurasa rasmi za mitandao ya kijamii na kutangaza kuwa atakaribishwa rasmi kama mchezaji wao tarehe 20 Juni, 2022.
“Tumeimarisha kikosi chetu kwa kumsajili mmoja wa mabeki bora katika soka la dunia baada ya mchezaji huyo wa kimataifa wa Ujerumani kujiunga na klabu hiyo akitokea Chelsea.
“Alikuwa kiungo muhimu wa timu hiyo ya London iliyonyanyua Ligi ya Mabingwa, Ligi ya Europa, Kombe la Dunia la Klabu, UEFA Super Cup na Kombe la FA. Pia ameshiriki katika Timu bora ya Ligi ya Mabingwa katika misimu miwili iliyopita,” Real Madrid ilieleza.
Rudiger anatazamiwa kushiriki mechi zake za kwanza na Real katika msimu wa 2022/23 ambao utang’oa nanga mwezi Agosti.
Leave a comment