CHAMA cha ACT-Wazalendo, kimesema Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, anakwamishwa na baadhi ya watendaji wake, hasa waliopewa dhamana ya kusimamia michakato ya uchaguzi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo Jumapili tarehe 23 Mei 2021, na Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo, Ado Shaibu, akizungumza na MwanaHALISI Online kwa simu, kuhusu chaguzi ndogo zilizofanyika tarehe 16 Mei 2021, kwenye majimbo ya Buhigwe na Muhambwe, mkoani Kigoma na kata tano .
Katika chaguzi hizo, ACT-Wazalendo kilichuana vikali na Chama Cha Mapinduzi (CCM), pasina kufua dafu baada ya chama hicho tawala kutwaa majimbo na kata zote.
Kwenye chaguzi hizo, waliogombea Jimbo la Muhambwe ni, Dk. Florence Samizi (CCM) na Julius Masabo (ACT-Wazalendo). Na Buhigwe, Galula Kudra (ACT-Wazalendo) na Mwalimu Eliadory Kavejuru (CCM) .
Akizungumzia uchaguzi huo, Ado amesema kuna dosari kadhaa zilijitokeza hasa Jimbo la Buhigwe, ambazo chama hicho kinaimani kwamba, Rais Samia hakuagiza zitokee.
Katibu Mkuu huyo wa ACT-Wazalendo ametaja dosari hizo kuwa ni, uwepo wa kura za kughushi na wasimamizi kuondolewa katika vituo vya kupigia kura.
“Katika Kata ya Ligoma iliyoko Tunduru Kusini ,tumefanikiwa kukamata karatasi za kupigia kura, tuliziwasilisha kwa wasimamizi wasaidizi hawakutupa ushirikiano, na hata wakati wa kuhesabu kura, kura nyingi ziliunganishwa pamoja,” amesema Ado.
Kufuatia dosari hizo, Ado amemuomba Rais Samia, achunguze malalamiko ya ACT-Wazalendo, ili abaini ukweli wake.
“Mimi naimani haya si aina ya mambo Rais Samia anaweza kuyapenda, anaweza akachunguza na kujua ukweli. Kama akichunguza atabaini haya tunayosema ni ukweli kuhusu uchaguzi, wako wanaomkwamishawanamrudisha nyuma Rais Samia,” amesema Ado.
MwanaHALISI Online imemtafuta Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Dk. Wilson Mahera, kwa ajili ya ufafanuzi wa tuhuma hizo, lakini hajatoa ushirikiano.
Leave a comment