RAIS Samia Suluhu Hassan amewaagiza wakuu wa mikoa ya Dar es Salaam, Amos Makala; Mkuu wa mkoa wa Pwani, Abubakar Kunenge na Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira (DAWASA) kwenda kusafisha mto Ruvu ambao ndio chanzo cha maji yanayoelekezwa kwenye mitambo ya uchakataji maji yanayotumika katika mikoa hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Pia amewaagiza kwenda kufungua vizuizi ambavyo baadhi ya wakulima wakubwa wameweka na kufunga mashine za kusukuma maji kwenda kwenye mashamba yao hususani ya wageni pamoja na mabwawa ya samaki kinyume cha taratibu.
Rais Samia ametoa maelekezo hayo leo tarehe 1 Novemba, 2022 katika Kongamano la Kitaifa la Nishati Safi ya Kupikia linalofanyika kwa siku Novemba 1-2, 2022 jijini Dar es Salaam.
Amesema mabadiliko ya tabia nchi yana sura mbili- kimungu na yale yaliyofanywa na binadamu kwa kuharibu vyanzo vya maji kuelekea kwenye mto Ruvu.
“Sasa nawaagiza mkuu wa mkoa Dar, Pwani pia Dawasa mhakikishe mmekwenda kuondoa vizuizi vyote, Dawasa walisema wamefanya mwezi uliopita lakini wanaweza kuwa wamerejea kwani binadamu ndivyo tulivyo.
“Kwa njia yoyote nataka mkasafishe mto Ruvu mtiririko wa maji uende sawasawa. Kama mtaenda kwa miguu, helikopta au magari sijui! nataka mkasafishe mto maji,” ameagiza.
Aidha, Rais Samia amesema matumizi ya mkaa na kuni yamesababisha uharibifu mkubwa wa misitu kwa kukata miti ya asili huku ya Pwani, Morogoro, Tabora, Lindi na Ruvuma ikiongoza.
Amesema nishati safi inakwenda sambamba na mambo ya mazingira hasa ikizingatiwa upatikanaji wa maji Dar es salaam umekuwa changamoto kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa na tabia nchi.
Leave a comment