BUNGE la Tanzania limeahirishwa kwa dharura leo Alhamisi tarehe 2 Juni 2022 kwa muda wa nusu saa kuanzia saa 4:00 asubuhi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Mwenyekiti wa Bunge, David Kihenzile ameahirisha Bunge hilo wakati Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Catherine Magine akianza kuchangia bajeti ya wizara ya nishati na madini kwa mwaka wa fedha 2022/23.
Wakati Magige akianza kuchangia, kuna sauti ya mbunge imesikika ikiomba mwongozo wa kiti cha spika na hakupewa nafasi lakini alikuwa akihoji kutokuwepo kwa mawaziri wa wizara hiyo, January Makamba na naibu wake, Stephen Byabato.
Hata hivyo, Mwenyekiti huyo wa Bunge, Kihenzile amesema, Serikali ipo hivyo akimtaka Magige kuendelea kuchangia.
Jambo hilo liliibua kidogo minong’ono na alionekana makatibu wa Bunge wakitoka walipokuwa wamekaa kwenda kwa mwenyekiti wa bunge kama mara mbili hivyo na baada ya sekundi kadhaa, Kihenzile akatangaza kuahirisha Bunge kwa dakika 30.
Baada ya muda huo wa nusu saa kumalizika, Bunge lilirejea baada ya mawaziri Makamba na naibu wake, Byabato kufika. Haijafahamika walichelewa wapi.
Leave a comment