VIJANA wa Wilaya ya Igunga mkoani Tabora, wameeleza kufaidika na fedha za mradi wa ujenzi wa madarasa na ofisi za walimu baada ya kununua pikipiki na kiwanja.
Vijana hao ambao ni mafundi ujenzi wa mradi huo katika Shule ya Sekondari Ziba wamesema hata baada ya ujenzi huo kukamilika sasa wamefanikiwa kujikwamua kiuchumi. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Wakizungumzia miradi hiyo kwa nyakati tofauti, Jongo Jilala na Richard Ernest wamesema hakika ujenzi huo umegusa maisha yao.
Jilala amesema hapo awali hali ilikuwa mbaya kiuchumi kwa kuwa hawakuwa na kazi za kufanya.
Amesema waliposikia Rais Samia Suluhu Hassan analeta hela za kujenga madarasa na vituo vya afya walipata matumaini kwani walifahamishwa kuwa watatumika mafundi wazawa.
“Tuliposikia hivyo, nilifarijika nikaomba na kubahatika kupata kazi, hela niliyopata ni nyingi lakini nimefanikiwa kununua pikipiki. Licha ya kwamba mradi umeisha lakini sasa bado naendelea kujikimu kimaisha,” amesema.
Wakati Richard Ernest amesema alikuwa na kiwanja ambacho alikuwa amelipia nusu lakini baada ya kufanya kazi hiyo alilipia fedha zilizobakia.
“Sasa nimemalizia malipo na nimesogeza ujenzi kidogo kwa hiyo namshukuru Rais Samia,” amesema Ernest ambaye yeye na wenzake walijenga madarasa matatu na ofisi ya walimu.
Aidha, Mkuu wa Shule ya Ziba, Ali Maulid amesema kwanza mradi huo umenufaisha jamii kwa watu kupata ajira.
“Lakini pili umetupunguzia msongamano wa wanafunzi darasani na tatu wanafunzi wanasoma katika mazingira mazuri.
“Tofauti na madarasa tuliyosomea sisi milango ilikuwa kila kona, mlango wenyewe, dirisha lilikuwa mlango lakini wanafunzi wa leo wanasomea kwenye madirisha ya vioo, madarasa yenye gypsum na umeme tumeshaweka,” amesema.
Leave a comment